Rais Samia ataka uchaguzi wa Serikali Mitaa usitie doa taifa

By Augusta Njoji , Nipashe
Published at 07:20 AM Oct 12 2024
Rais Dk. Samia Suluhu Hassan akijiandikisha kwenye Daftari la Wapigakura kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika Kitongoji cha Sokoine, Chamwino mkoani Dodoma jana.

RAIS Samia Suluhu Hassan amewataka Watanzania kuhakikisha uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajia kufanyika mwezi ujao, unamalizika salama bila kulitia doa taifa kwa kuwa ndio utakaoonesha taswira ya uchaguzi mkuu mwakani.

Amesisitiza umuhimu wa kuchagua viongozi wa ngazi ya serikali za mitaa na kueleza kuwa hata yeye anapokwama katika masuala yanayohitaji idhini ya Mwenyekiti wa Mtaa wake, humfuata mtaani.

Akizungumza jana baada ya kujiandikisha katika Daftari la Mpigakura Serikali za Mitaa katika Kitongoji cha Sokoine, wilayani Chamwino, mkoani hapa, Rais Samia alisema ni muhimu kila Mtanzania kudumisha amani na usalama katika uchaguzi huo bila kulitia doa taifa.

“Niwaombe sana mchakato ufanyike kwa usalama na kwa amani ili tusiitie doa nchi yetu, tumalize uchaguzi wa awali salama. Mchakato huu utatoa taswira ya uchaguzi mkuu ujao. Niwaombe wananchi tujitokeze tukachague vyema ili tupate sura halisi mbele tunakokwenda,” alisisitiza.

Rais Samia alisema kwa kuwa uchaguzi huo utafanyika siku ya Jumatano, itatangazwa baadaye wananchi wasiende kazini ili kushiriki kupiga kura.

“Kumekuwapo na mkanganyiko kati ya daftari hili na daftari la Tume Huru ya Uchaguzi. Haya ni madaftari tofauti, hivyo wananchi wajitokeze kwa wingi kujiandikisha na kushiriki kuchagua viongozi bora watakaowaongoza katika maeneo yao.

“Kuna ubabaifu unajitokeza wengine wanahisi akishajiandikisha kwenye daftari lile la Tume ya Uhuru ya Uchaguzi, hana haja ya kujiandikisha huku hapana.

“Tunajiandikisha kule kwa uchaguzi wa mwakani lakini hapa kwenye eneo lako unachagua mwenyekiti wako wa kitongoji na kamati yake na viongozi wengine. Ni  daftari lingine tofauti, kwa hiyo niwaombe wote kuanzia leo (jana) hadi Oktoba 20 mwaka huu, kila mmoja kwa nafasi yake ajitokeze kujiandikisha,” alisisitiza.

Kuhusu umuhimu wa uchaguzi huo, Rais Samia alisema viongozi watakaowachagua ndio watasaidia kuweka usalama na amani katika maeneo yao.

“Katika utambuzi wa watu kwenye maeneo yetu ni dhamana yao nani kaingia, nani katoka, nani anashughuri gani, nani hana, kesi ndogo ndogo wao wanaweka usalama wa maeneo yetu lakini kubwa la utambuzi,” alisema.

Rais Samia alisema kila mwananchi mwenye mahitaji mbalimbali katika eneo lake kuanzia kwa viongozi hao hata yeye amekuwa akienda kwa mwenyekiti wake.

“Hata mimi mbali na makuta (kuta) yale (Ikulu) kuna shida nyingine ni kijaza fomu ninaulizwa mwenyekiti wangu wa kijiji ni lazima nitoke kwenye makuta (yale), nimfuate nipate idhini yake na muhuri wake ili kupata huduma nyingine. Sasa jiulize usipokwenda kumchagua, ukachaguliwa ukawekewa ambaye hukudhania utawekewa.

“Tunapofanya shughuli zote za maendeleo hawa ndio wa kwanza katika maeneo yao tunawasukuma watoe watu washiriki, sasa akiwa mzembe utaanza kulalamika kiongozi mwenyewe ni mzembe, lakini hukwenda kumchagua. Ukienda kumchagua wewe na wenzako mtaweka mtu anayefaa kuwatumikia,” alisisitiza.

Rais Samia alisema uchaguzi huo ni uhuru wa demokrasia na tamaduni ambapo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka mfumo wa tawala za mikoa.

“Usiposhiriki unakiuka Katiba inayokuongoza ndani ya nchi yako, mfumo huu ni mfumo wa kikatiba na ni haki kwa kila mtu kushiriki kuchagua au kuchaguliwa.

“Kila anayeanzia miaka 21 mkimwona mzuri wa jinsia yoyote, anajituma, anasifa, anamwingiliano mzuri na watu na yupo mbele katika shughuli za maendeleo akijitokeza kuomba kuchaguliwa, basi mchagueni. Mmemwona anafaa lakini yupo nyuma hataki kwenda anaogopa kushindwa na mnahakikisha huyu mzuri atatusaidia msukumeni, mwambieni hebu nenda chukua fomu.

“Huu mchakato ni kila mwenye sifa anaomba tunachujana vizuri bila kupendeleana na wale wazuri tunaowaona hawa watatuongoza vizuri, basi tunawapeleka wakashindane na mmoja wao akiibuka ndio kiongozi wetu,” alisema.