Yanga yapewa onyo Ligi Kuu

By Adam Fungamwango , Nipashe
Published at 10:51 AM Oct 08 2024
Timu ya Yanga.
Picha: Mtandao
Timu ya Yanga.

KAMATI ya Uendeshaji na Usimamizi ya Ligi, ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB), imeipiga faini Klabu ya Coastal Union na kuionya Yanga kwa makosa ya kuchelewa kufika uwanjani.

Taarifa iliyotolewa jana na TPLB, imesema Klabu ya Yanga imepewa onyo kali kwa kosa la kuchelewa kufika kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam, kuelekea mchezo wao wa Ligi Kuu dhidi ya KMC ambao uliisha kwa wao kupata ushindi wa bao 1-0, Septemba 29, mwaka huu.

Katika taarifa hiyo ya TPLB imeeleza kuwa Yanga ilifika uwanjani saa 1:48 usiku, badala ya saa 1:30 usiku na hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:15 ya Ligi Kuu kuhusu taratibu za mchezo.

Imeeleza adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu taratibu za mchezo.

Klabu ya Coastal Union, imetozwa faini ya Sh. milioni moja, kwa kosa la kuchelewa kuiwasilisha orodha ya wachezaji na maofisa wa ufundi kuelekea kwenye mchezo wao dhidi ya Mashujaa FC, uliochezwa, Septemba 13, mwaka huu, Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam, kinyume cha matakwa ya Kanuni ya 17:6, huku adhabu ikitolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62, mchezo huo ambao ilifungwa bao 1-0.

Coastal, pia imepewa onyo kwa kosa la kuchelewa kuwasilisha listi ya wachezaji, benchi la ufundi na viongozi wake kuelekea kwenye mchezo wa Ligi Kuu kati ya timu hiyo dhidi ya KMC, Agosti 29, mchezo uliomalizika kwa sare ya bao 1-1, mechi ilipigwa, KMC Complex, Mwenge.

Taarifa ilieleza timu hiyo iliwasilisha orodha yake saa 7:50 mchana, badala ya saa 7:00 mchana kama ilivyoainisha kwenye Kanuni ya 17:6, adhabu ikitolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62.

Nayo, Tabora United, imepigwa faini ya Sh. milioni moja, kwa kushindwa kujumuisha wachezaji angalau wawili wa timu za vijana kwenye kikosi chao katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya KenGold uliomalizika kwa kufungana bao 1-1.

Kamati hiyo imesema Tabora United imerudia kosa hilo katika michezo minne licha ya kukumbushwa mara kadhaa kufanya hivyo.