WANAKWAYA watano wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), wamefariki dunia papo hapo na wengine 20 kujeruhiwa vibaya, baada ya basi dogo aina ya Toyota Costa kuacha njia na kupinduka katika eneo la Kirinjiko Airtel, Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni, leo Oktoba 22,2024, amesema basi hilo limepata ajali majira ya alfajiri, wakati likitokea Jijini Dar es Salaam kuelekea Machame, Wilaya ya Hai kwenye shughuli za maziko ya mwanakwaya mwenzao.
Kwa mujibu wa DC Mgeni, basi hilo liliacha njia na kugonga kalavati dogo la Kirinjiko.
"Ni kweli watu watano wamepoteza maisha, wakiwamo wanawake watatu na wanaume wawili. Wote hawa ni wana kwaya KKKT waliokuwa wakitokea Dar es Salaam kuelekea Machame,"amesema.
Basi hilo lilikuwa likiongozana na mabasi mengine manne, na dereva wake alisinzia na ghafla alishtuka ameligonga kalavati hilo.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED