Profesa Mkumbo avutiwa na utendaji wa Bandari ya Dar

By Joseph Mwendapole , Nipashe
Published at 03:11 PM Oct 22 2024
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo akiwa katika ziara bandari ya Dar es Salaam leo ambapo aliongea na viongozi wa Mamlaka ya Bandari TPA na DP World.
Picha:Mpigapicha Wetu
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo akiwa katika ziara bandari ya Dar es Salaam leo ambapo aliongea na viongozi wa Mamlaka ya Bandari TPA na DP World.

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Profesa Kitila Mkumbo, amepongeza uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na kampuni ya kimataifa ya uwekezaji ya DP World katika bandari ya Dar Es Salaam.

Amesema serikali itaendelea kuboresho zaidi bandari hiyo katika maeneo mbalimbali ikiwemo makusanyo ya kodi kupitia Dira ya Taifa ya miaka 25 ijayo (2050).

Aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kikazi bandari hapo ambapo alisema uwekezaji uliofanyika katika bandari ya Dar es Salaam ni mkubwa na una tija katika taifa katika maeneo mbalimbali ikiwemo ukusanyaji wa mapato na ufanisi mkubwa katika utoaji wa huduma na kuvutia wafanyabiashara zaidi kutumia bandari hiyo.

“Nikiwa Waziri mwenye dhamana katika sekta ya uwekezaji na mipango nimeamua kuitembelea bandari ya Dar es Salaam ili kujionea utendaji wake kazi kupitia uwekezaji mkubwa uliofanyika,” alisema

“Kkwakweli nimefurahishwa sana na uboreshaji uliofanyika katika kimiundombinu na kiutendaji yaliyofanyika na haya ni matunda ya uwekezaji huu,” alisema

Aliipongeza menejimenti na uongozi wa (TPA) kwa usimamizi mzuri na mipango mbalimbali inayoendelea katika upanuzi wa bandari ya Dar es Salaam na bandari nyingine ambayo itasaidia kukuza uchumi wa nchi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo akiwa katika ziara bandari ya Dar es Salaam leo ambapo aliongea na viongozi wa Mamlaka ya Bandari TPA na DP World.

Alisema kupitia mipango ya Dira Maendeleo ya Taifa , Serikali inapenda kuona ni namna gani uwekezaji huo utazidi kuwa na tija katika miaka 25 ijayo kupitia mipango na mikakati mbalimbali ambayo Serikali imeipanga.

Alisema uboreshaji unaoendelea kufanyika katika bandari hiyo kupitia uwekezaji uliofanyika utachochea uwekezaji katika sekta mbalimbali hapa nchini kama vile sekta ya viwanda mbalimbali, sekta ya kilimo na sekta ya elimu, ambazo zote zitasaidia kuleta tija kwa nchi ikiwemo kutoa ajira na kukuza uchumi.

“Namshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu uwekezaji huu mkubwa na wa kihistoria kwa nchi yetu,  kwani hivi sasa tumeanza kuona matunda yake,” alisema Waziri Mkumbo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo akiwa katika ziara bandari ya Dar es Salaam leo ambapo aliongea na viongozi wa Mamlaka ya Bandari TPA na DP World.

Katika ziara hiyo Waziri Mkumbo alibainisha namna uwekezaji huo utakavyoweza kukuza uchumi hasa katika mipango ya nchi ya muda mfupi na mipango ya muda mrefu na kuona kuwa yana tija kwa pande zote mbili, akimaanisha upande wa serikali na upande wa mwekezaji.

Kampuni ya kimataifa ya DP World imepewa kuwekeza kwenye gati namba 4 mpaka 7, hivyo na tangu ianze kazi  imesaidia kuongezeka kwa mapato baada ya kuboresha miundombinu mbalimbali pamoja na kuweka gati na kupakua mizigo kwa muda mfupi sana tofauti na ilivyokuwa zamani.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo akiwa katika ziara bandari ya Dar es Salaam leo ambapo aliongea na viongozi wa Mamlaka ya Bandari TPA na DP World.