MUHAS kuendesha kambi maalum ya uchunguzi wa afya kwa wananchi

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 05:48 PM Feb 24 2025
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Prof Appolinary Kamuhabwa (katikati) akitoa maelezo kwa mwandishi wa habari kuhusu kongamano la kumbukizi ya Kansela wa kwanza wa MUHAS hayati Dk Ali Hassan Mwinyi.

Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kimeandaa kambi maalum ya uchunguzi wa afya kwa wananchi, itakayofanyika katika Kampasi ya Mloganzila kuanzia Februari 26 hadi 27, 2025, kuanzia saa 3:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni.

Akizungumza na waandishi wa habari, Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Appolinary Kamuhabwa, amesema kambi hiyo inalenga kutoa uchunguzi wa magonjwa mbalimbali, yakiwemo macho, masikio, pua na koo, kinywa na meno, saratani ya matiti na shingo ya kizazi, homa ya ini, pamoja na tezi dume kupitia vipimo vya damu.

Aidha, sambamba na uchunguzi huo, wataalamu wa MUHAS watatoa elimu kuhusu madhara ya matumizi holela ya dawa na usugu wa dawa mwilini, magonjwa ya kuambukiza, utengenezaji na ukarabati wa vifaa tiba, uchakataji wa taarifa za afya kwa kutumia akili mnemba, pamoja na lishe bora.

Prof. Kamuhabwa ameongeza kuwa kutakuwa na maonyesho maalum ya afya na elimu, yakionesha mafanikio katika sekta ya afya na elimu, zikiwemo tafiti mpya, ubunifu wa kiteknolojia, na juhudi zinazofanywa na MUHAS katika kuboresha huduma za afya nchini.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Prof Appolinary Kamuhabwa (katikati) akitoa maelezo kwa mwandishi wa habari kuhusu kongamano lijalo la kumbukizi ya Kansela wa kwanza wa MUHAS Aliyekuwa Rais wa Tanzania Dk Ali Hassan Mwinyi linalotarajiwa kuchezwa Ijumaa wiki hii katika Kampasi ya Mloganzila jijini Dar es Salaam. Kutoka kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi Prof Raphael Sangeda na kushoto ni Prof Nahya Masoud.
“Washiriki watapata fursa ya kujifunza na kushuhudia jinsi teknolojia mpya inavyoboresha utoaji wa huduma za afya na elimu. Pia, kutatolewa huduma mbalimbali za uchunguzi wa afya bila malipo,” amesema Prof. Kamuhabwa.

Katika kuimarisha mazingira ya mafunzo, huduma za afya na tafiti, MUHAS pia itaweka jiwe la msingi kwa ujenzi wa Ndaki ya Tiba (College of Medicine) na Shule ya Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) katika Kampasi ya Mloganzila.

“Mradi huu ni hatua muhimu katika kupanua miundombinu ya chuo, kuongeza udahili wa wanafunzi, na kuboresha ubora wa mafunzo kwa wanataaluma wa sekta ya afya,” ameongeza Prof. Kamuhabwa.