Morogoro walilia ubora wa barabara

By Christina Haule , Nipashe
Published at 05:03 PM Feb 06 2025
Meneja wa TARURA, Mhandisi Emmanuel Ndyamukama (mwenye shati la pinki), akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), juu ya ujenzi wa barabara hiyo unaotarajia kuanza mwaka huu
Picha: Christina Haule
Meneja wa TARURA, Mhandisi Emmanuel Ndyamukama (mwenye shati la pinki), akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), juu ya ujenzi wa barabara hiyo unaotarajia kuanza mwaka huu

WANANCHI wa Kata ya Lukobe, Manispaa ya Morogoro, wameiomba serikali kuona umuhimu wa kujenga barabara ya Kilombero-Mazimbu Farm kwa viwango bora, ili kukabiliana na changamoto ya kujaa maji.

Wamesema barabara hiyo wakati wa mvua za masika hukatisha mawasiliano, kwa saa kadhaa, na kuwasababishia maafa na kuwarudisha nyuma uchumi wao.

Wananchi hao walisema hayo jana, wakati wakiongea na vyombo vya habari, kutokana na mvua za masika inayotarajia kuanza.

Diwani wa Kata ya Lukobe, Selestine Mbilinyi, akizungumzia na waandishi wa habari (hawapo pichani), juu ya adha wanayoipata wakazi wa kata hiyo, huku akiomba barabara hiyo kujengwa mapema
Diwani wa Kata hiyo, Selestine Mbilinyi, aliwataka Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA), kujenga barabara hiyo mapema, bila kusubiria madhara yanayoweza kujitokeza. 

Mmoja wa wananchi hao, dereva wa bajaji, Frank Alpakshard, aliiomba serikali iweke miundombinu rafiki kwenye barabara hiyo, ili kuifanya kuwa salama wakati wote na kuwaepusha na adha ya kuharibu vifaa vyao vya moto na kuingia gharama za matengenezo.

Getruda Cosmas, ni mkazi wa mtaa wa Tushikamane, aliiomba serikali kuona umuhimu wa kuwajengea barabara kwa haraka, ili kuwaepusha kushindwa kwenda kazini kwa siku kadhaa, kutokana na mvua na barabara kutopitika na kulazimika kuvuka kwa miguu kwenye maji mengi na hivyo kuhatarisha afya zao.

Wananchi wa Kata ya Lukobe, wakivuka maji katika eneo la Kwa Bwana Jela, lililopo barabara ya Kilombero-Mazimbu Farm, kwa kuongozwa na askari wa Kikosi cha Uokojai na Zimamoto, wakitumia kamba iliyowekwa JWTZ, kwa ajili ya kuvukia ili wasisombwe na maji hayo kwenye mafuriko ya mwezi Januari mwaka 2024
Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Ndyamukama, aliwataka wakazi wa Kata ya Lukobe, kutambua kuwa serikali imeshaanza usanifu kwa ujenzi wa barabara hiyo na baada ya usanifu itajengwa kwa kiwango cha lami, huku ikizingatia vigezo vya ujenzi wa eneo lenye maji.

Anasema ujenzi wa barabara hiyo, utasaidia kudhibiti maji mengi yanayotoka kwenye maeneo na wilaya za jirani na milima inayozunguka eneo hilo na kuwaondolea wananchi changamoto zinazowakabili mara kwa mara.