Simbachawene awataka wananchi kujitokeza uchaguzi serikali za mitaa

By Timothy Itembe , Nipashe
Published at 08:31 PM Oct 03 2024
Waziri George Simbachawene (mwenye skafu) na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Patrick Chandi Marwa wakisalimiana kwa furaha wilayani Serengeti leo Oktoba 3, 2024.
Picha: Mpigapicha Wetu
Waziri George Simbachawene (mwenye skafu) na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Patrick Chandi Marwa wakisalimiana kwa furaha wilayani Serengeti leo Oktoba 3, 2024.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumiaji wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene, amesisitiza umuhimu wa wananchi wenye umri wa kuanzia miaka 18 kujitokeza kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Akizungumza leo Oktoba 3,2024 katika mkutano wa hadhara kijijini Kemakorete, Waziri Simbachawene amewataka vijana na wananchi kwa ujumla kushiriki katika uchaguzi huo, ili kuhakikisha wanapata viongozi wapenda maendeleo.

Waziri ameongeza ni muhimu wananchi wapige kura ili kuepusha kuchaguliwa kwa viongozi wasiopenda maendeleo, akisema kuwa viongozi hao wanajulikana.

Waziri amehudhuria uwekaji wa jiwe la msingi kwa mradi wa Shule ya Msingi Komote na mradi wa maji Kemakorete.

Mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evans Mtambi, alieleza kuwa chini ya utawala wa Rais Samia Suluhu Hassan, mkoa wa Mara umepokea zaidi ya Sh. trilioni 1.2 kwa ajili ya miradi mbalimbali.

Mbunge wa Viti Maalumu, Esther Matiko, amemuomba serikali kuongeza kasi ya ajira za walimu, hasa wa sayansi, kipaumbele wale wanaojitolea li kukabiliana na upungufu katika shule.