Mahakama yamgomea Naibu Rais Kenya

By Vitus Audax , Nipashe
Published at 03:16 PM Oct 16 2024
Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua.
Picha: Mtandaoni
Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua.

MAHAKAMA ya Rufani nchini Kenya chini ya jopo la majaji watatu imekataa kuingilia kati mchakato wa kuondolewa madarakani kupitia ombi la kuzuia mchakato huo.

Aidha, mahakama hiyo imesema mchakato huo utaendele kama ulivyopangwa bila kuingiliwa ba mamlaka hiyo kwa sasa.

Mahakama iliyoketi mapema leo Jumatano Oktoba 16,2024 ilikataa kutoa maagizo ya kusitisha kesi ya kushtakiwa kwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua katika Bunge la Seneti.

Majaji Erick Ogolla, Antony Mrima na Frida Mugambi wamesema hakuna suala lolote litakalomkuta Gachagua,  iwapo Bunge la Seneti litaendelea na hoja ya kumtimua katika wadhifa huo.

Hata hivyo, Majaji hao wamesema uamuzi huo haumuzuii Gachagua kukata rufani kuupinga katika korti nyingine kama hatoridhika nao na pia mahakama bado inaweza kuamua matokeo ya mchakato wa Bunge.

Wakijibu uamuzi huo, timu ya wanasheria wa Gachagua imetaka kurekebisha ombi hilo kulingana na kile ambacho kinaweza kushuhudiwa katika Bunge la Seneti.

Wanasheria hao wakiongozwa na Lempaa Soyinka wamesema malalamiko yaliyorekebishwa hayatakuwa mapya na hakuna upande utakaobaguliwa, bali walalamikiwa wanataka kuchelewesha kesi kwa kukataa marekebisho yetu.

Upande wa wajibu maombi ukiongozwa na Benson Milimo, wakili wa Bunge la Kitaifa alipinga ombi hilo akitoa mfano kuwa uamuzi huo hautakuwa wa haki ikiwa hawatafahamu undani wa marekebisho hayo.

Uamuzi huo wa mahakama unaweka msingi wa kesi ya kumuondoa Gachagua kwenye nafasi yake kuendelea katika Seneti ambako Bunge la Seneti litajadili kesi hiyo kwa siku mbili kabla ya kupiga kura ya kumuondosha au kumbakisha rasmi katika ofisi yake ya Naibu Rais.

Mapema leo Oktoba 16,2024 Gachagua aliwasili katika Bunge la Seneti kwaajili ya kusikiliza mwendelezo wa majadiliano pamoja na kutoa utetezi wake lililoanza majira ya saa nne asubuhi huku lilionekana kuzingirwa na ulinzi mkali wa polisi nchini humo pamoja na usalama upande wa Naibu Rais.

Matokeo ya mchakato huo yanatarajiwa kulifanya bunge la nchi hiyo kuketi tena siku ya Ijumaa kujadilili na kupendekeza jina la mtu mwingine ambaye atachukua nafasi ya Gachagua kama Bunge la Seneti itaridhia kuondolewa kwake.