Kocha Inter Z'bar atolea sababu kipigo

By Hawa Abdallah , Nipashe
Published at 08:23 AM Sep 08 2024
ull-time
JKU 3- 1 INTER ZANZIBAR
Kofi hamza 07. Abdillah hassan 15
Neva kaboma 65
Tariki Mohammed 89
Picha:Mtandao
ull-time JKU 3- 1 INTER ZANZIBAR Kofi hamza 07. Abdillah hassan 15 Neva kaboma 65 Tariki Mohammed 89

KOCHA wa timu ya Inter Zanzibar FC, Abrahaman Mohamed amesema kupoteza mchezo wao wa kwanza wa Ligi kuu ya Zanzibar juzi kumetokana na ugeni wao kwenye Ligi hiyo.

Inter Zanzibar FC ilijikuta  ikipokea kichapo cha mabao 3-1 kutoka kwa bingwa mtetezi, JKU SC, katika mchezo uliochezwa  juzi katika uwanja wa New Amaan Complex Visiwani hapa.

Akizungumza na gazeti hili, Mohamed alisema walicheza na timu yenye uzoefu mkubwa katika soka la Zanzibar lakini pia iliyopata kucheza mashindano mawili ya kimataifa hivi karibuni 'klabu Bingwa na Kagame cup'.

Alisema kupitia mashindano hayo walifanikiwa kupata maandalizi mazuri ya kujiandaa  na msimu hivyo matokeo aliyoyapata hayawezi kumshangaza.

Alisema wachezaji wake walicheza vizuri katika kipindi cha kwanza lakini kipindi  cha pili walishindwa kwenda sawa na wapinzani wao na kujikuta wakipata kipigo hicho.

"Wapinzani wetu walicheza kwa mipango kwa kutumia uzoefu wao ndani ya ligi jambo ambalo wachezaji wangu walishindwa kwenda nao sawa, tumefungwa kwa sababu ya ugeni wetu kwenye Ligi," alisema Mohamed.

Aidha alisema mbali na ugeni wa Ligi lakini pia wachezaji wake wengi walikuwa na hofu ya mchezo jambo lilowafanya kushindwa  kucheza  vizuri.

"Mchezo huu hatukufanya vizuri lakini kupitia mchezo huu nimeona mapungufu yapo wapi hivyo katika mchezo wetu wa pili dhidi ya Malindi SC tutakuwa bora zaidi," alisema.

Hata hivyo alisema kuwa kazi iliyombele yake katika kukiboresha kikosi chake ni kuhakikisha anawatoa uoga na hofu ya mchezo bila kujali historia ya timu wanayocheza nayo.