Wananchi wamesisitizwa kutunza vyanzo vya maji

By Marco Maduhu , Nipashe
Published at 05:00 PM Aug 13 2024
Wananchi wamesisitizwa kutunza vyanzo vya maji.
Picha:Marco Maduhu
Wananchi wamesisitizwa kutunza vyanzo vya maji.

WANANCHI wa kijiji cha Masabi Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama,wamesisitizwa kutunza vyanzo vya maji ili waendelee kupata huduma ya majisafi na salama.

Hayo yamebainishwa leo Agosti 13,2024 na kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Godfrey Mnzava, alipofika kukagua uendelevu wa mradi wa upanuzi wa skimu ya maji, kutoka Segese hadi kijiji cha Masabi,ambapo chanzo chake ni kisima kirefu.

Amesema wananchi wanapaswa kuitunza miradi ya maji ambayo inazinduliwa na Mwenye wa Uhuru,pamoja na kutunza vyanzo vya maji ili  kuwa na uhakika wa maji, na kuendelea kuhudumiwa kwa kupata majisafi na salama.

Aidha, amesema kazi ya mwenge wa uhuru pia ni kukagua uendelevu wa miradi ya maji ambayo tayari ilishapitiwa na mwenge  wa uhuru kipindi cha nyuma, ili kuona huduma ambazo zinaendelea kutolewa kwa wananchi, pamoja na kuongeza mtandao na kufikia wananchi wengi zaidi kwa kupata huduma ya majisafi na salama na kumtua ndoo kichwani mwanamke.

“Huduma ya maji haina mbadala, na kama kauli yenu ya RUWASA inavyosema “Ruwasa maji bombani” endeleeni kusambaza maji zaidi kwa wananchi, ikiwamo kuwaunganishia majumbani mwao na kumtua ndoo kichwani mwanamke,”amesema Mnzava. 

“Mwenge wa Uhuru upo tayari kuona huduma za maji ambazo zinatolewa kwa wananchi katika kijiji hiki cha Masabi,” ameongeza.

Awali Meneja Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Kahama Mhandisi Maduhu Magili, akisoma taarifa ya mradi huo, amesema umetekelezwa na watalaamu wa ndani wa Ruwasa kwa mfumo wa “Force Account” kwa lengo la kutatua kero ya muda mrefu ya ukosefu wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi wa kijiji hicho.

“RUWASA tunaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji,na upanuzi wa mradi huu umenufaisha wananchi wa kijiji cha Masabi wapatao 2,400 na gharama zake ni Sh.milioni 64.6”amesema Mhandisi Magili.

Nao wananchi wa kijiji hicho cha Masabi, wameishukuru Serikali kupitia RUWASA kwa kuwatekelezea mradi huo wa maji safi na salama, hali ambayo imewaondolea adha ya kufuata maji umbali mrefu, na kwamba baadhi yao tayari wameshavuta maji majumbanimwao na wengine wakiendelea kuchota kwenye vituo.