TFS Rufiji watoa mizinga ya nyuki vikundi 38

By Julieth Mkireri , Nipashe
Published at 10:20 AM Apr 26 2024
news
Picha: Julieth Mkireri
Mbunge wa Jimbo la Rufiji Mohamed Mchengerwa kulia ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) akiwa akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge (kushoto) na Meneja wa TFS Rufiji Francis Kiondo.

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Rufiji wamekabidhi mizinga ya nyuki ya kisasa 300 kwa Mbunge wa Rufiji Mohamed Mchengerwa kwa ajili ya vikundi 38.

 Walikabidhi mizinga hiyo kwa Mchengerwa ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI)  kutekeleza ombi la vikundi hivyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi mizinga hiyo Meneja wa TFS Wilaya ya Rufiji Francis Kiondo alisema mizinga hiyo itawasaidia vijana kujiimarisha kiuchumi na kuondokana na utegemezi pamoja na kuepuka kuingia kwenye biashara za mkaa.

Kiondo ambaye amekabidhi mizinga hiyo kwa niaba ya Kamishina wa Uhifadhi TFS  Dos Santos Silayo amesema kila kikundi kitapata mizinga ya nyuki ya kisasa kumi ambayo inauwezo wa kuzalisha asali kilo 20 za asali kwa mwaka.

Akipokea Mizinga Mchengerwa ameshukuru Wizara ya Maliasil na  Utaliii pamoja na  TFS kwa kuwezesha vijana mizinga hiyo ambayo itasaidia kuinua uchumi kwa wananchi wa jimbo hilo la Rufiji.

Pia ameishukuru Taasisi hiyo kwa ushirikiano waliotoa kipindi cha mafuriko kwa kutumia boti zao kubebea wananchi walipko maeneo ya bondeni , kutoa vyakula na maturubali kwa waathirika.