Waziri Mhagama awataka wazazi/walezi kutenga muda malezi ya watoto

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 01:20 PM May 06 2024
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Jenista Mhagama.
Picha: Mpigapicha Wetu
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Jenista Mhagama.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Jenista Mhagama ambaye pia ni Mbunge wa Peramiho amewataka wazazi kutenga muda kwa ajili ya malezi ya watoto ili kuwatizama na kurekebisha mienendo yao.

Kauli hiyo ameitoa wakati aliposhiriki kama mgeni rasmi maadhimisho ya miaka 69 ya Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Songea Vijijini, sherehe zilizofanyika katika Kijiji cha Kilagano katika Halmashauri ya Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma.

Waziri amesema, mtoto anayelelewa kwa kuangalia mfano mzuri wa baba na mama lazima atakuwa na nidhamu na tabia njema.

"Wazazi tukae tutafakari utaratibu tunaotumia kulea watoto wetu ili wawe na madili bora katika katika Jamii,"alibanisha.

Ameeleza kwamba lengo la kuanzishwa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi ni kuhakikisha inajenga maadili mema ndani ya chama na taifa kwa ujumla.

Niendelee kuhimiza Viongozi wa jumuiya ya wazazi ndani ya wilaya kwenye Kata na kwenye matawi na kwenye mashina tuendelee kulibeba jukumu hili.

"Kizazi kilichopo na hata kizazi kipya kimeathirika na maswala ya utandawazi, na nguvu mpya ya mawasiliano kama isipotumika vizuri itakuwa ni chanzo cha upotofu wa maadili.Tunahitaji wanachama wenye maadili, tunahitaji wananchi wa Peramiho wenye maadili, alifafanua." alisema Waziri Mhagama.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea Vijijini, Menace Komba ameishukuru Serikali na juhudi za Mbunge, Jenista Mhagama, walizofanya za kurekebisha Mpaka wa Mlima Lihanje.

Tulifanya Mkutano na timu ya Mawaziri na tulifanya Mkutano Kilagano na kuzungumza na wananchi na baadae kufanikiwa kurekebisha mipaka ya Mlima Lihanje.

"Serikali ya wilaya itahakikisha  wananchi walioathirika na zoezi hilo kwa kuondolewa kwenye Mlima na kuwarudisha chini wanapata ardhi iliyotengwa kwa usawa," alisema.