Nishati safi ya kupikia italeta mageuzi ulindaji wa mazingira- Mahundi

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 02:09 PM Oct 01 2024
Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Maryprisca Mahundi akipika kwa kutumia gesi.

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Maryprisca Mahundi amesema nchi inakwenda kushuhudia mageuzi makubwa ya utunzaji wa mazingira kupitia Mkakati wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambao kinara wake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk. Samia Suluhu Hassan.

Mahundi ameyasema hayo Jijini Dodoma  wakati akihamasisha wananchi kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi na kuanza kupika kisasa kupitia nishati safi ya kupikia.

"Tunaposema tutunze mazingira, tunaweza kuona takriban hekta 469,000 za misitu zinateketea kwa mwaka  sababu ya shughuli mbalimbali za binadamu ikiwemo matumizi ya nishati zisizo safi za kupikia (kuni na mkaa) hivyo tunapotumia nishati safi kupikia tunaenda kutunza mazingira yetu." ameeleza Mahundi

Amesema mbali ya uharibifu wa mazingira ambao umekuwa ukitokea kutokana  na matumizi ya nishati isiyo safi lakini pia kumekuwa na athari kwa watumiaji hasa kuathirika mfumo wa upumuaji kutokana na moshi mwingi.

1

Ameongeza kuwa, zaidi ya watanzania 33,000 hupoteza maisha  kila mwaka kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi.

Ameeleza kuwa,  katika matumizi ya nishati safi ya kupikia kama vile gesi na umeme kila aina ya chakula kinaweza kupikwa na kutilia mkazo kuwa nishati safi ya kupikia si anasa bali inaenda kulinda afya za watumiaji pamoja na mazingira.