Naibu Waziri Kapinga ambananisha mkandarasi mbele ya wananchi

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 09:47 AM Jul 03 2024
Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga akimbananisha mkandarasi mbele ya wananchi.

Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga amewataka wakandarasi wote wanaotekeleza miradi ya usambazaji wa umeme vijijini kuhakikisha wanatekeleza miradi hiyo kwa wakati na kwa ubora.

Naibu Waziri ametoa maelekezo hayo jana wakati akiwa katika ziara yake mkoani Shinyanga iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya Umeme Vijijini katika majimbo ya mkoa huo huku akimtaka mkandarasi wa kampuni ya Tontan kuhakikisha anafikisha umeme katika vijiji vya Buganzo na Gulla ili malengo ya serikali ya kuhakikisha wanawasha umeme kwa vijiji vyote hapa nchini yanatimia.

“Ndugu zangu, tumefika hapa kwa ajili ya kuongelea masuala ya maendeleo. Mkataba kati ya Serikali ya Awamu ya Sita na wananchi wake ni maendeleo. Leo tumefika ndugu zangu kuongelea maendeleo na miradi iliyo chini ya sekta yetu ya nishati hususani miradi ya umeme.

Wananchi wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga hayupo pichani.

Miradi hii ya umeme inafanyika kwenye kila kijiji cha nchi hii. Ni uwekezaji mkubwa sana ambao Mhe. Rais, Dk. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi ya wananchi wake. Nimeambiwa kwenye Kata hii kuna Vijiji vitano, na vijiji vitatu vimeshawashwa umeme na viwili bado. Na sisi tutahakikisha umeme unawake,” amesisitiza Naibu Waziri Kapinga.