Kesi ya uhujumu uchumi kunguruma leo

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 10:08 AM May 06 2024
Bango la  Mahakama ya Wilaya ya Arusha.
Picha: Maktaba
Bango la Mahakama ya Wilaya ya Arusha.

KESI ya uhujumu uchumi inayowakabili watumishi watatu wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha na kuisababisha serikali hasara ya Sh.milioni 64.2, itaanza kutajwa leo katika Mahakama ya Wilaya ya Arusha mkoani hapa.

Washtakiwa hao wanaokabiliwa na mashtaka tisa ni Amani Mlay, Gerson Mollel na mmiliki wa Kampuni ya Usambazaji  Vifaa vya Umeme na Mabomba, Cecy Zumba.  

Kesi hiyo inasikilizwa na Hakimu Mkazi, Devotha Msofe. Kwa mujibu wa  Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Sifael Mshana, mshtakiwa wa kwanza (Mlay), anashtakiwa kwa matumizi mabaya ya nyaraka, kumdanganya mwajiri wake kuhusu dokezo lenye ombi la kiasi hicho cha Sh. milioni 64.2 zinahitajika kwa ajili ya vifaa vya umaliziaji wa ujenzi wa uzio wa Shule ya Msingi Shangarao iliyopo Kata ya Muivaro.

 Katika maelezo ya kosa katika nyaraka hiyo ilikuwa ikionyesha Cecy Electrical Plumbing Co. Ltd, iliomba  Sh. milioni 64.2.

 Katika kosa la pili la matumizi  ya nyaraka yenye maelezo ya uongo kutoka kwa Cecy, yakionyesha amewasilisha nyaraka yenye manunuzi ya nondo 500 zenye ukubwa milimita 12 na  nondo 500 za milimita 8.

 Manunuzi mengine ni malori saba ya kokoto, sita ya mchanga, mifuko 350 ya saruji, matofali 4,000 na wilbaro moja.

 Kosa la tatu ni kumdanganya mwajiri wake kuwa Mei 25 mwaka jana kwa kutoa nyaraka ya uongo ya  madai ya malipo, ikionyesha anadai  Sh. milioni 64.2.

Kosa la nne, ni matumizi mabaya ya nyaraka yenye muhtasari wa kikao  cha kamati ya usimamizi wa mradi wa umaliziaji wa ujenzi wa jengo hilo, huku akijua si kweli.

Kosa la tano, linamkabili Cecy Zumba kwa kusaidia kutenda uhalifu, ambapo anadaiwa kutenda kosa kati ya Mei 1 hadi Desemba mwa jana. 

Kosa la sita, linamkabili Cecy na Mollel, kumsaidia Mlay kufanya uhalifu kwa kutumia nyaraka za uongo kwa ajili ya kumdanganya mwajiri wake kusaini zilizotokana na kikao. 

Kosa la nane, ni wizi  kwa watuhumiwa wote, kati ya Mei 1 hadi Desemba mwaka jana.  

Vilevile, kosa la tisa linawakabili washtakiwa wote na  kuisababishia mamlaka hasara.