Gamondi aanika siri ushindi Yanga

By Faustine Feliciane , Nipashe
Published at 09:12 AM Sep 24 2024
Gamondi aanika siri ushindi Yanga
Picha:Mtandao
Gamondi aanika siri ushindi Yanga

KOCHA wa Yanga, Miguel Gamondi, amesema matokeo mazuri wanayoyapata yanatokana na mtindo wake wa kubadilisha badilisha wachezaji kwenye kikosi chake cha kwanza.

Jumamosi Yanga ikicheza katika Uwanja wa New Amaan Complex visiwani Zanzibar, ilitinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kutoa kipigo cha mabao 6-0 dhidi ya CBE ya Ethiopia, hivyo kufuzu kwa jumla ya mabao 7-1, kutokana na ushindi wa bao 1-0 iliyoupata wiki moja kabla ugenini.

Akizungumza na Nipashe juzi, Gamondi alisema ugumu wa ratiba ya ligi na mashindano ya kimataifa yanamfanya kutumia wachezaji tofauti tofauti katika kila mchezo.

"Hii ni faida ya kuwa na kikosi kipana, kila mchezaji anayepata nafasi anafanya kile ninachokitarajia, ratiba yetu ni ngumu sana, ni lazima tufanye 'rotation' (mzunguko) ya wachezaji," alisema Gamondi.

Alisema anafanya hivyo ili kuwapa muda wa kupumzika na kujiandaa kwa mchezo unaofuata katika kila ratiba ya timu hiyo msimu huu.

"Naangalia mahitaji ya timu kwa wakati huo, mfano kwenye mchezo wetu dhidi ya CBE kule Zanzibar kuna wachezaji walianzia benchi na kuwapa nafasi wachezaji wengine, nilimtumia Nkane kama beki wa pembeni na alifanya vizuri alipoingia, unaona naweza nikaanza na Nzengeli [Max], Chama [Clatous] na Pacome [Zouzoua], nje wapo akina Aziz Ki, Prince Dube na Musonda, ratiba za michezo yetu inalazimu kufanya hivi," alisema Gamondi.

Katika hatua nyingine, Gamondi, amesema kwa sasa wanaelekeza nguvu zao kwenye michezo yao ya Ligi Kuu baada ya kufanikiwa kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

"Tunarejea kwenye ligi, lazima tuwe makini kwa sababu ligi si nyepesi, unaweza kuona namna timu zilivyojiandaa, natarajia ushindani mkubwa, akili zetu lazima tuzielekeze huko tukisubiri kujua wapinzani wetu kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika," alisema Gamondi.

Droo ya hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho Afrika inarajiwa kuchezeshwa Oktoba 7, mwaka huu jijini Cairo, Misri yalipo Makao Makuu ya Shirikisho la Soka Afrika, CAF.

Baada ya droo hiyo wawakilishi wa Tanzania kwenye mashindano hayo, Yanga na Simba zitawafahamu wapinzani wao kwenye michuano hiyo.

Kwa upande wa watani wao wa jadi, Simba ambao wanaiwakilisha nchini kwenye Kombe la Shirikisho Afrika, nayo imetinga hatua ya makundi baada ya kuitupa nje Al Ahli Tripoli ya Libya kwa jumla ya mabao 3-1, ushindi ambao waliupata katika Uwanja wa Benjamin Mkapa juzi, hii ikiwa ni baada ya mchezo wa kwanza uliochezwa Libya wiki moja kabla kumalizika kwa sare tasa.