Chama cha ACT Wazalendo kimeanzisha mpango wa kuchangisha wananchi kwa ajili ya kugharamia kampeni za uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika tarehe 27 Novemba 2024.
Katibu Mkuu wa Chama hicho Ado Shaibu amesema hatua hiyo ni mwendelezo wa utamaduni wa Chama hicho kuwashirikisha wadau wa demokrasia kwenye masuala yote makubwa ya uendeshaji wa Chama.
"Tumekuwa tukiwashirikisha wadau na wananchi kwa ujumla kwenye chaguzi zote na programu zote kubwa za Chama ikiwemo Mikutano Mikuu ya Chama na ziara za kitaifa" amesisitiza Ado na kuongeza;
"Kama ilivyo desturi yetu, michango yote itaendeshwa kwa uwazi na matumizi yake yatatolewa taarifa ya wazi kwa umma baada ya uchaguzi. Kama mnavyojua, Chama chetu kinaendeshwa kwa uwazi na ndio chama kisafi zaidi katika usimamizi wa fedha kwa mujibu wa Ripoti za Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) na ukaguzi unaofanywa kila mwaka na Msajili wa Vyama vya Siasa".
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED