MKUU wa Chuo Cha Bahari Dar es Salaam (DMI) Dk.Tumaini Gurumo amesema serikali imeona upo umuhimu wa kuongeza jitihada za kuwekeza zaidi katika chuo hicho kwa kununua vifaa vya kisasa vya kufundishia, ili kufungua ajira zaidi kwa Watanzania ndani na nje ya nchi.
Akizungumza jana jijini Arusha katika banda la maonyesho la chuo hicho, Dk.Tumaini alisema fursa zipo nyingi kwenye usafirishaji majini,ndani na nje ya nchi,hivyo jitihada za uwekezaji zinazofanyika katika chuo hicho, zitasaidia kuounguza uhaba wa ajira nchini.
"Tunaishukuru serikali kuwekeza fedha nyingi katika ununuzi wa mitambo mikubwa ya kisasa ya kufundishia kutoka nje ya nchi, ambapo mmoja umeshawasili chuoni hapa na mmoja upo njiani kuwasili na vifaa mbalimbali vya utoaji elimu tumenunua,"alisema.
Aidha alisema kwa ujumla sekta ya uchukukuzi na usafirishaji majini kuna fursa kubwa za ajira, kutokana na uhaba wa wataalamu, hali inayosukuma DMI kwa kushirikiana na serikali kufanya jitihada kubwa kuzalisha wataalamu.
"Ambapo kwa sasa chuo hicho kutokana na maboresho mbalimbali yanayofanyika kimefanikiwa kuongeza idadi ya wanafunzi kutoka 8000 hadi kufikia 12,000 mwaka huu,"alisema
Alisema sekta ya usafirishaji kwa njia ya maji ina fursa kubwa ya ajira ndani na nje,hivyo vema kuendelea kuwekeza kwa kuboresha chuo hicho.
Aidha alisema chuo hicho kwa kuahirikiana na serikali kinapambana kwenda na ulimwengu kwa kuhakikisha wanakua na vifaa vyabkisasa vya ufundishaji ili kutoa elimu itakayosaidia kukidhi mahitaji ya soko la ndani na kimataifa.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED