BRELA yatanua wigo usajili wa biashara na leseni

By Pilly Kigome , Nipashe
Published at 02:39 PM Apr 25 2024
Wafanyakazi wa BRELA wakimuhudunia mwananchi aliyetembelea banda lao katika maonesho ya Miaka 60 ya Muungano jijini Dar es Salaam.
Picha: Pili Kigome.
Wafanyakazi wa BRELA wakimuhudunia mwananchi aliyetembelea banda lao katika maonesho ya Miaka 60 ya Muungano jijini Dar es Salaam.

WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni(BRELA) imewataka Wazanzibar kutumia vyema fursa za kidijitali katika usajili wa biashara na leseni pasipo kufika makao makuu

Hayo yamesemwa na Afisa Leseni Mwandamizi Brela, Rehema Kionomela alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho ya Miaka 60 ya Muungano jijini Dar es Salaam.

Kionomela, amefafanua BRELA inasimamia sheria sita kati ya hizo sheria ya leseni ya viwanda inasimamia Muungano kwa kuhudumu Tanzania Bara na Zanzibar.

Amesema kwa sasa BRELA imeboresha mifumo yake mingi ikiwemo mfumo wa usajili kupitia  njia ya mtandao (ORS) ambapo mteja anatakiwa kutengeneza akaunti na kuingiza taarifa zake popote alipo.

Amesema kupitia mfumo huo na ule wa TNGP mteja anaweza akafanya chochote kusajili biashara au leseni popote alipo pasipo na ulazima wa kusafiri kufata huduma hizo.

“ Katika kuadhimisha Miaka 60 ya Muungano hasa kipindi hiki cha awamu ya sita Brela imepiga hatua kubwa sana tofauti na awali ambapo mifumo ilikuwa hakuna hasa kuwarahisishia wazanzibar kupata huduma pasipo kusumbuka” amefafanua

Nelson Mwambo mkazi wa Chanika mmoja wa aliyetembelea banda la BRELA aliiambia Nipashe kuwa, katika taasisi za serikali zinazotendea haki wateja ikiwemo na BRELA kutokana na uboreshaji wa huduma zao.

Amesema alifika asubuhi ya saa3 hadi kufika saa nne tayari ameshakamilishiwa huduma zote ambazo amekuja kuzifanya katika banda hilo.

“Nimefurahishwa na huduma na uboreshaji wa huduma nawasihi wafanyabiashara wasifanye biashara zao kiholela waje wasajili biashara na alama zao pasipo usumbufu wowote” amefafanua Mbwambo