WAKAZI 189,000 kufikiwa mradi maji Ziwa Victoria

By Shaban Njia , Nipashe Jumapili
Published at 04:40 PM Feb 23 2025
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa (katikati), akifurahia baada ya kukata utepe kuzindua vifaa vya ujenzi wa mradi wa maji ya ziwa Victoria. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha na kushoto Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel
Picha: Shaban Njia
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa (katikati), akifurahia baada ya kukata utepe kuzindua vifaa vya ujenzi wa mradi wa maji ya ziwa Victoria. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha na kushoto Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel

WAKAZI 189,936 wa halmashauri ya Ushetu, mkoani Shinyanga, wanatarajia kunufaika na mradi wa maji wa Ziwa Victoria na kuondokana na magonjwa ya mlipuko ya kuhara na homa ya matumbo.

Mradi huo unatarajiwa kukamilika Oktoba, mwakani 2026. Unatekelezwa na Mkandarasi Sihotech Engineering Co. Ltd ya jijini Dar es Salaam, kwa kushirikiana na Kampuni ya Mpole Construction and Co. Ltd ya Iringi.

Utagharimu  Sh. bilioni 44 huku kazi zisizohitaji ujuzi wakipewa vijana wa kata mradi utapopita.

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Shinyanga, Mhandisi Julieth Payovela, ameyabainisha hayo leo, wakati wa hafla fupi ya kukabidhii mabomba kwa mkandarasi kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, umeshafikia asilimia tatu ya utekelezaji wake.

Amesema, mradi unatekelezwa ndani ya miezi 24 na utakapokamilika utahudumia wakazi 189,936 kutoka kata 11 na vijiji 54 kati ya 20 na vijiji 58 na utakuwa umeongeza asilimia 85 ya upatikanaji wa maji katika halmashauri hiyo.

Amezitaja kata hizo kuwa ni Igunda, Kisuke, kinamapula, Nyamilangano, Mapamba, uyogo, Bukomela, Ukune, Mpunze, Ushetu na Ulowa, utasaidia kupunguza magonjwa ya mlipuko ya kuhara, kipundupindu na homa ya matumbo.

189,000 kufikiwa mradi maji Ziwa Victoria
Payovela amesema, utasaidia kupunguza mimba na ndoa za utotoni mashuleni kwa wanafunzi wa kike, walikuwa wakitumia muda mwingi kutafuta huduma ya maji umbali mrefu na kukutana na vishawishi njiani na mpaka sasa umefikia asilimia tatu ya utekelezaji.

Mkazi wa Ulowa, Tihan Stephen, amesema wanatumia maji ya kwenye visima ambavyo wamechimba kwenye makazi yao na wamekuwa wakiugua homa ya matumba mara kwa mara hasa watoto na kuiomba serikali kumsisitiza mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji wake, ili ukamilike na waondokane na magonjwa hayo.

189,000 kufikiwa mradi maji Ziwa Victoria
Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, amesema licha ya kuwa na maji ya Ziwa Victoria, kwa wilaya ya Kahama, kwa zaidi ya miaka 15 wakazi wa jimbo hilo, waliendelea kukabiliwa na tatizo la ukosefu wa huduma safi na salama na kutumia maji ya visima na kuumwa matumbo.