Igunga na matarajio kuwasili Katibu Itikadi, Uenezi

By Neema Emmanuel , Nipashe Jumapili
Published at 01:41 PM Feb 15 2026
Wananchi wakiwa pemebezoni mwa barabara kusubiri ujio wa kiongozi huyo
Picha: Neema Emmanuel
Wananchi wakiwa pemebezoni mwa barabara kusubiri ujio wa kiongozi huyo

Wananchi wa Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, wameeleza matarajio yao kufuatia ujio wa Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenan Kihongosi, anayetarajiwa kuwasili wilayani humo, leo

Akizungumza na Nipashe Digital, Daudi Shamduli, mkazi wa Kata ya Mbutu wilayani Igunga, amesema ujio wa kiongozi huyo, umeamsha matumaini mapya kwa wananchi, wakiamini utakuwa fursa ya kusikiliza na kutatuliwa kwa changamoto zinazowakabili.

Ameeleza kuwa wananchi wamehamasika kujitokeza kwa wingi ili kumsikiliza, wakiamini kuwa ziara hiyo italeta majibu ya masuala mbalimbali ikiwemo kilimo, barabara na ufugaji.

“Tunajitokeza kwa wingi kumsikiliza kwa kuwa tuna imani ujio wake utatutatulia matatizo yetu, yakiwemo ya kilimo, barabara na ufugaji,” alisema Shamduli.

Zakaria Kisama, mkazi wa Igunga, amesema ujio wa huo, ni matarajio makubwa kwa wananchi wa wilaya hiyo, akisisitiza kuwa wanaamini changamoto zao zitapatiwa ufumbuzi.

Amesema wamejitokeza kwa wingi kumsikiliza kiongozi huyo kwa matumaini kuwa ujio wake utaleta mabadiliko chanya na maendeleo katika wilaya ya Igunga.