HOSPLAN kwa kushirikiana na Kituo cha Saratani kutoka nchini India (Apollo), imefanya kongamano kwa wataalam wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kuhusu matumizi ya dawa zinazotibu saratani ya damu na uvimbe, ambazo huwapo sehemu mbalimbali mwilini.
Saratani aina hiyo ni nyingi ikilinganishwa na saratani za damu.
Akizungumza wakati wa kongamano hilo, Mtaalam wa Saratani za Damu Kituo cha Saratani Apollo Mumbai-India, Dk. Punit Jain, amesema dawa hizo ambazo zinasaidia kutibu wagonjwa wa saratani ya damu, zitawasaidia wataalam kutoa huduma bora.
“Tupo Tanzania na madaktari pamoja na wataalam waliobebea katika saratani ya damu, dhumuni letu hasa ni kuleta huduma za kisasa kwa kubadilishana ujuzi na hospitali za Tanzania, ili kuleta huduma za kibingwa na ubingwa bobezi zilizo bora,” amesema Dk. Jain.
Mratibu wa wa Huduma za Afya Hosplan-Tanzania, Dk. Nimrod Mtangwa, amesema katika kuhakikisha utoaji wa huduma bora kwa wagonjwa wa saratani, Hosplan imeandaa makongamano na kambi mbalimbali za afya, ambazo zitasaida wataalam wa saratani nchini kubadilishana uzoefu na wataalam wa ugonjwa huo kutoka India.
Bingwa wa Magonjwa ya Saratani Dk. Heri Tungaraza, amesema dawa hizo mpya ambazo zimeboreshwa kwa ajili ya wagonjwa wa saratani, ni bora na zinafanya kazi vizuri na pia madhara yake ni madogo zaidi ikilinganishwa na huduma ya kemotherapi.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED