Naibu Katibu Mkuu wa chama cha ACT Wazalendo Bara, Ester Thomas amesema ACT Wazalendo imejipanga vyema kuhakikisha wanachama wake waliotia nia kugombea kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wanapata msaada wa kisheria katika kipindi cha uhitaji.
Alisema maneno hayo jana Oktoba 23 Jijini Mwanza wakati akizungumza na watia nia wa mitaa ya majimbo ya Nyamagana na Ilemela.
"Madhali umetia nia kugombea kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Naomba simama imara, usitetereke, usiwe na hofu na wala usikubali kutishwa. Chama kiko pamoja na wewe. Pia tuna Wanasheria; ambao wako tayari kukusaidia wakati wowote." alisema Ester
Aidha Ester aliwakumbusha watia nia hao dhima na wajibu wa Mwenyekiti wa Mtaa kwenye maendeleo ya mtaa. Amesema kwenye mitaa na vijiji ndiko wanakoishi wananchi na huko ndiko inapopita na kufanyika miradi ya maendeleo.
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji utafanyika Novemba 27, 2024 na ACT Wazalendo ni miongoni mwa vyama vinavyokwenda kushiriki uchaguzi huo.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED