Mnyama ametinga hatua ya 32 bora ya mashindano ya Kombe la FA baada ya kuifunga Greenland FC kutoka mkoani Kagera mabao 3-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Meja Isamuhyo, Dar es Salaam leo.
Wekundu wa Msimbazi walienda mapumziko wakiwa mbele kwa mabao 2-0.
Mabao ya Simba katika mechi hiyo yalifungwa na Baraka Mwangosi, Antony Mligo na Neo Maema.
KMC FC imetolewa katika mashindano hayo baada ya kukubali kufungwa penalti 3-2 na Bandari Tanzania kutoka mkoani, Mtwara.
Timu hizo zilimaliza dakika 90 kwa sare ya mabao 3-3, mechi ikichezwa kwenye Uwanja wa KMC Complex.
Fountain Gate pia imesonga mbele katika michuano hiyo baada ya kuifunga Mapinduzi bao 1-0 huku Coastal Union ikiwaondoa Nyumbu kufuatia ushindi wa mabao 3-1 wakati Biashara United ya Mara wakishindwa kufika uwanjani kuwakabili Mbeya City ya Mbeya.
Hatua ya 64 bora ya mashindano hayo itamalizika kesho kwa michezo 18 kuchezwa kwenye viwanja tofauti nchini, ambapo mabingwa watetezi, Yanga watawakaribisha Cosmopolitan ya Dar es Salaam.
Bingwa wa mashindano hayo hupata tiketi ya kushiriki michuano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Afrika.
© 2026 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED