Waziri Lukuvi, ahimiza Vyama vya Siasa kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 08:50 PM Oct 07 2024
Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Fransis Mutungi akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi alipotembelea Makao makuu ya Chama cha ACT Wazalendo Jijini Dar es Salaam.
Picha:Mpigapicha Wetu
Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Fransis Mutungi akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi alipotembelea Makao makuu ya Chama cha ACT Wazalendo Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi amewahamasisha na kuwahimza viongozi wa Vyama vya Siasa juu ya umuhimu wa kushiriki katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Waziri amesema hayo wakati alipotembelea ya Makao Makuu Vyama Vinne vya Siasa leo Oktoba 07, 2024 katika ziara yake iliyolenga kuendelea kuimarisha mahusiano na falsafa ya Rais. Dk, Samia Suluhu Hassan ya 4R.

Amesema lengo ni kuvifikia vyama vyote 19 kabla ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ikiwa ni pamoja na kutoa salamu za upendo za Rais Dk. Samia na kuwapa pongezi viongozi wapya waliochaguliwa hivi karibuni.

“Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unasimamiwa na TAMISEMI na una kanuni na taratibu  za uendeshaji wake zinazohusisha Vyama vya Siasa, hivyo natumia fursa hii kuhimiza wananchi wote kujitokeza kujiandikisha katika zoezi linaloanza tarehe 11-20 /10/2024 kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ili wapate nafasi ya kuchagua na kuchaguliwa” amesema Waziri Lukuvi.

Aidha amewaomba viongozi wa kisiasa kuendelea kutoa ushauri kwa Serikali bila kusubiri vikao vya baraza vinavyoitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa na badala yake wanaweza kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kama kiungo ili waweze kuishauri Serikali wakati wowote.

Waziri Lukuvi amesema; “Ni wajibu wetu kudumisha amani na upendo kama alivyotuasa Mhe. Rais kwa kushindanisha sera zetu kwa hoja na tukishapata matokeo tuwachie waliochaguliwa ambao watakuwa ni Wenyeviti wa vijiji, Wenyeviti wa Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji watekeleze wajibu wao.Nashukuru sana kwa sababu vyama vyote wamekubali kutembelewa kwa ratiba ambayo itakuwa imepangwa,"

Kwa upande wake, Doroth Temu Makamu Mwenyekiti wa Chama cha ACT amesema wao kama wadau wanaendelea na kazi ya msingi ya kuelimisha uma juu ya umuhimu wa uchaguzi  na kuendelea kuwasilisha Serikalini maoni yote wanayoyapata kwa wananchi.  

“Tutaendelea kuwakumbumbusha wananchi kwamba uchaguzi ni jukumu muhimu:  na kuwahimiza kushiriki kwao kama raia wa Tanzania katika kuchagua viongozi nasi tukitegemea uchaguzi kuwa huru na wakuaminika,” amesema Doroth Temu.

Ikumbukwe kwamba katika siku ya kwanza ya ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) ametembelea na kukutana na Viongozi wa Vyama vya CHAUMMA, ACT Wazalendo, CCK na  UPDP.