TRC kuongeza safari za treni za SGR Dar-Moro

By Frank Monyo , Nipashe
Published at 03:36 PM Jul 01 2024
Treni ya SGR.

Shirika la Reli Tanzania (TRC) limetoa mabadiliko ya ratiba na ongezeko la safari za treni za SGR zinazofanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Morogoro kuanzia Julai 5, 2024.

Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Julai Mosi, 2024 na kusaini na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano, Jamila Mbarouk imeeleza ongezeko la safari hizo litahusisha kuanza kwa treni mpya ya haraka (express train) ambayo itakuwa ikifanya safari kati ya Dar es Salaam na Morogoro bila kusimama vituo vya kati.

Aidha, mabadiliko ya ratiba yatakuwa kama ifuatavyo; Treni ya haraka itakuwa ikiondoka Dar es Salaam saa 12:00 asubuhi na saa 1:10 usiku. Treni itaondoka Morogoro saa 12:20 asubuhi na saa 1:30 usiku.

Pia, treni ya kawaida itakuwa ikiondoka Dar es Salaam saa 3:30 asubuhi na saa 10:00 jioni na itaondoka Morogoro saa 3:50 asubuhi na saa 10:20 jioni.

Vilevile, TRC imewashauri abiria kukata tiketi kwa njia ya mtandao au madirisha ya tiketi yaliyo ndani ya vituo vya treni saa 2 kabla ya muda wa safari, ili kuepuka msongamano.