Shinyanga yaji-'mwambafai' kulinda tuzo ya usafi

By Marco Maduhu , Nipashe
Published at 09:17 PM Feb 08 2025
Meya wa Manispaa ya Shinyanga Elias Masumbuko akiongoza kikao cha Baraza la madiwani.
Picha: Marco Maduhu
Meya wa Manispaa ya Shinyanga Elias Masumbuko akiongoza kikao cha Baraza la madiwani.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Shinyanga, imejipanga kuimarisha hali ya usafi wa mazingira, ili kulinda tuzo ya usafi ambayo ilishinda kutoka Wizara ya Afya.

Hayo yamebainishwa jana, kwenye Kikao cha Baraza la Madiwani cha Robo ya Pili, wakati wa uwasilishwaji wa taarifa ya Kamati ya Mipango Miji na Mazingira.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Revocatus Lutunda, alibainisha hayo wakati akijibu swali alililoulizwa na Diwani wa Kizumbi, Rubeni Kitinya, juu ya uimarishaji wa usafi wa mazingira katika manispaa hiyo.

Amesema, ili kuendelea kulinda hadhi ya manispaa hiyo kuwa mji safi na kulinda tuzo, wameweka mikakati madhubuti ya kuendelea kuimarisha hali ya usafi zaidi, pamoja na kukumbusha wananchi kufanya usafi katika maeneo yao.

“Suala la usafi kwa kweli katika mji wetu tumelegalega hali siyo nzuri, lakini tumeweka mikakati ya kuimarisha usafi zaidi, kukumbusha wananchi kufanya usafi, pamoja na kutenga siku maalumu ya kuwa tunafanya usafi, ili kuendelea kulinda heshima ya tuzo yetu ya usafi wa mazingira,” amesema Lutunda.

Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Elias Masumbuko, naye amesisitiza suala la usafi kwenye mji huo na kwamba, uchafukwa sasa umeanza kuoneka na jitihada zinahitajika, ili kuendelea kulinda heshima yao ya kupata tuzo ya ushindi wa usafi wa mazingira ngazi ya miji.

Diwani wa Kizumbi, Rubeni Kitinya
Diwani wa Kizumbi, Kitinya, aliuliza swali juu ya mikakati ambayo Manispaa ya Shinyanga, imechukua dhidi ya kuimarisha hali ya usafi wa mazingira, kwa sasa hali imeanza kuwa siyo nzuri kutokana na maeneo mengi kuwa machafu.

Amewalalamikia pia mawakala wa kukusanya uchafu, kuwa wameshindwa kufanya kazi zao vizuri, huku wakati wa kupeleka taka dampo, baadhi huagushwa hovyo barabarani na kusababisha mji kuonekana mchafu.