OFISA Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Prof.William Pallangyo amesema Oktoba 12, 2024 Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua Mradi wa ujenzi wa Chuo cha TIA kampasi ya Mwanza amao ujenzi wake umefikia asilimia 99.
Prof.Pallangyo ametoa kauli hiyo jana wakati Waziri wa Fedha Dk.Mwigulu Nchemba alipotembelea na kukagua ujenzi wa chuo hicho baada ya kuanza rasmi ziara yake ya siku saba mkoani Mwanza.
“Majengo haya yaliyogharimu zaidi ya Sh.bilioni 7.8 yana uwezo wa kubeba wanafuzi 2430 ukilinganisha na wanafunzi 750 waliokuwa wakihudumiwa katika majengo ya awali na mradi huu umetusaidia kupata majengo ya kudumu na kutoka katika majingo ya kukodi ambayo yalikuwa hayakidhi ongezeko la wanafunzi,” alisema Prof.Pallangyo.
Kuhusu miradi ya TIA nchini, Prof.Pallangyo alisema zimetolewa zaidi ya Sh.bilioni 58.1 kwa lengo la kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia katika kampasi zote.
Waziri Dk.Mwigulu Nchemba akizungumza mara baada ya ukaguzi wa chuo hicho alisema hatua hiyo ni miongoni mwa shughuli zinazoendelea kutekelezwa na serikali katika kuboresha sekta ya Elimu.
Alisema chuo hicho kutasaidia kuongeza mzunguko wa fedha pamoja na kuleta faida zaidi kwa wakazi wa maeneo jilani.
Katika hatua nyingine Waziri Dk.Mwigulu akifanya Mkutano wa hadhara wilayani Misungwi na kupokea kero ya uhaba wa maji pamoja na malipo ya fidia kwa Wananchi.
Dk.Nchemba alieleza kupokea kero hizo na kuahidi kuendelea kutoa fedha katika miradi hiyo ambayo tayari inaendelea kutekelezwa.
Aidha aliwataka wakazi wa Misungwi kuwa na umoja kwa kufuata R4 alizoziasisi Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuvumiliana na kushirikiana katika usimamizi na utekelezaji miradi muhimu.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED