Mongella awataka wana CCM kutembea vifua mbele

By Marco Maduhu , Nipashe
Published at 08:20 PM Sep 06 2024
Naibu Katibu Mkuu wa CCM bara John Mongella akizungumza na wajumbe na viongozi wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini.
Picha:Marco Maduhu
Naibu Katibu Mkuu wa CCM bara John Mongella akizungumza na wajumbe na viongozi wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini.

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara John Mongella, amewataka wana CCM kutembea vifua mbele, kujivunia mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Chama hicho kwa wananchi, chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

2Mongella ambaye pia ni mlezi wa CCM Mkoa wa Shinyanga, amebainisha hayo leo Septemba 6,2024 wakati akizungumza na wajumbe na viongozi  mbalimbali wa chama cha mapinduzi CCM wilaya ya Shinyanga Mjini.

Amesema kutokana na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuitendea haki ilani ya uchaguzi wa chama cha mapinduzi CCM, na kutekeleza miradi mingi ya maendeleo kwa wananchi, hivyo wanaCCM wanakila sababu ya kutembea vifua mbele kujivunia mafanikio hayo.

“Wana CCM tunakila sababu ya kutembea vifua mbele, kujivunia mafanikio ya utekelezaji wa ilani ya CCM kwa wananchi,sababu miradi mingi ya maendeleo imetekelezwa na mingine bado inaendelea kutekelezwa, na tusikae kimya kuitangaza miradi hii bali tuendelee kuinadi,”amesema Mongella.

“Hapa Shinyanga ni ngome ya chama cha mapinduzi CCM, na Mkoa huu unakwenda kupata mafanikio makubwa ya kimaendeleo, na miradi mingi imetekelezwa ambapo uwanja wa ndege Ibadakuli una historia ndefu lakini sasa una kwenda kukamilika, na pia kuna miradi mikubwa ya maji inatekelezwa,”ameongeza Mongella.

Aidha, amesema kutokana na utekelezaji wa ilani ya CCM kwa asilimia kubwa kwa wananchi, Chama hicho kina kwenda kushinda kwenye chaguzi zote.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa, akizungumza kwenye mkutano huo, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi mkoani humo na kutekelezwa miradi mingi ya maendeleo.

Amesema shukrani ambayo watampatia Rais Samia kama mkoa wa Shinyanga, ni kumpatia ushindi wa kishindo kwenye uchaguzi wa Serikali za mitaa mwaka huu, na uchaguzi mkuu mwakani 2025.

“Maua ambayo tunampatia Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na kuleta fedha nyingi za miradi ya maendeleo hapa shinyanga, tutapiga kura za kujaa kwenye gunia la “rumbesa” na tunafurahi kutupatia walezi wa Chama ambao ni ngazi za juu,”amesema Mabala.

Mongella yupo mkoani Shinyanga akiendelea na ziara yake ya kuimarisha Chama pamoja na kuzungumza na wananchi kwenye mikutano ya hadhara.