Waziri wa Madini Anthony Mavunde ameainisha mpango wa serikali wa kusaidia utatuzi wa changamoto zinazowakabili wachimbaji wadogo nchini ikiwamo kuwekeza zaidi katika utafiti wa kina kugundua uwepo wa madini katika maeneo mbalimbali ili kuwaongoza vizuri wachimbaji hao.
Mavunde ameyasema hayo leo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti maalumu (CCM), Dk. Christine Ishengoma ambaye amehoji mpango wa serikali kuwasaidia Wachimbaji Wadogo wa Madini Wilaya ya Ulanga.
Akijibu swali hilo. Waziri Mavunde amesema mpango wa serikali kuwasaidia wachimbaji hao ni utoaji wa Leseni za uchimbaji kwa wachimbaji wadogo;Kutoa elimu ya matumazi ya teknolojia sahihi ya uchimbaji ili kuongeza tija.
Pia, amesema huduma ya uchorongaji kwa gharama nafuu kupitia Shirika la Madini Tanzania (STAMICO);Upatikanaji wa mikopo nafuu kwa wachimbaji kupitia Benki mbalimbali na Taasisi za fedha na fursa ya ukodishaji wa mitambo na vifaa chini ya usimamizi wa STAMICO kupitia makampuni yaliyoingia makubaliano(MoU) na STAMICO.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED