Wizara yakazia kuwanoa walimu sekondari

By Grace Mwakalinga , Nipashe Jumapili
Published at 04:06 PM Feb 16 2025
Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Sera, Utafiti na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Emmanuel Kilundo akisaini kitabu cha wageni katika Shule ya Sekondari ya Ufundi Mtwara
Picha: Grace Mwakalinga
Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Sera, Utafiti na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Emmanuel Kilundo akisaini kitabu cha wageni katika Shule ya Sekondari ya Ufundi Mtwara

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, imesema itaendelea kutoa mafunzo endelevu kwa walimu kazini, na kuwafikia wote wanaofundisha masomo ya sayansi na hisabati, kwa shule za sekondari nchini.

Mafunzo hayo yanahusisha mbinu mbalimbali za ufundishaji, ikiwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama), kwa lengo la kuboresha ufundishaji na kuongeza ufanisi katika masomo hayo.

Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Sera, Utafiti na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Emmanuel Kilundo, ameyasema hayo, alipotembelea kituo cha mafunzo, kwa walimu wa masomo ya sayansi na hisabati katika Shule ya Sekondari ya Ufundi Mtwara yakiwahusisha walimu kutoka mikoa ya Njombe, Lindi na Mtwara.

Amesema mafunzo hayo endelevu, yatasaidia walimu kuboresha ufanisi wao kazini na kutumia teknolojia katika ufundishaji, jambo ambalo linatarajiwa kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu hususan masomo  ya sayansi na hisabati.

Mwalimu wa somo la Kemia, Jimmy Ngao ( kushoto) akionesha jaribio la utengenezaji wa kemikali mbalimbali mbele ya Mkurugenzi Msaidizi anayeshughulikia Sera, Utafiti na Ubunifu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Emmanuel Kilundo ( wa tatu kushoto)wakati wa mafunzo kwa walimu wa masomo ya Sayansi na Teknolojia yanayofanyika Shule ya Sekondari ya Ufundi Mtwara, mwingine kulia mwalimu Alice Mngaya
“Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, inatumia mbinu hizi za kisasa kama sehemu ya juhudi za kuondoa changamoto zilizokuwapo katika ufundishaji wa masomo ya sayansi na hisabati na kuhakikisha kuwa, wanafunzi wanapata elimu bora inayozingatia maendeleo ya sayansi na teknolojia,” amesema Kilundo.

Kuhusu utekelezaji wa mafunzo hayo, Kilundo amesema kuwa wanawajengea uwezo wathibiti ubora wa shule, ambao watasaidia kusimamia mifumo ya ufuatiliaji, ili kuhakikisha kuwa mbinu zinazotolewa zinatekelezwa ipasavyo shuleni. 

“Wathibiti ubora, baada ya kupata mafunzo maalum, watafuatilia utekelezaji wa mbinu hizo kwa karibu, kuhakikisha kuwa wanafunzi wanapata elimu  inayozingatia viwango vya ubora,” amesema Kilundo.

Ameongeza kuwa mbinu nyingine ya upimaji wa mafunzo hayo, ni kupitia mitihani inayotolewa na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), matokeo yatasaidia kupima kiwango cha uelewa  na ufaulu kwa wanafunzi.

Msimamizi wa Kituo cha Mtwara, Majaliwa Mkalawa akifafanua namna mafunzo yanavyoendeshwa kwa walimu
Akizungumzia motisha kwa walimu wa masomo hayo waliopata mafunzo watapokea vyeti vya kutambua ushiriki wao, kuhamasisha kufanya vizuri zaidi, ili kupata fursa nyingine za mafunzo zinapotokea.

Ameongeza kuwa serikali imeanza kutekeleza Sera  mpya ya Elimu ya Mwaka 2014 Toleo la 2023 na mitaala iliyoboreshwa, ambao unalenga kushughulikia changamoto kwenye masomo ya sayansi na hisabati.Anasema miongoni mwaka ni ukosefu wa mbinu za kisasa za ufundishaji, upungufu wa vifaa vya kufundishia kama maabara, matumizi duni ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama), na ukosefu wa mafunzo endelevu kwa walimu kazini (MEWAKA).

Amesema mtaala ulioboreshwa,  unalenga  kumjengea uwezo mwanafunzi kutumia maarifa, stadi na mitazamo chanya katika maisha ya kila siku.

 “Mafunzo haya yanatarajiwa kuleta mabadiliko makubwa katika mfumo wa elimu nchini, wanafunzi wengi watahamasika kusoma masomo haya, kwa sababu yatafundishwa kwa mbinu rahisi na nyepesi, hivyo kushawishi wanafunzi kuyapenda.”

Mwenyekiti wa Wawezeshaji katika Mafunzo ya Walimu wa Masomo ya Sayansi na Hisabati, ambayo yanaratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kupitia Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari nchini (SEQUIP).

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) Idara ya Sayansi, Hisabati na Teknolojia (STEM), Dk. Absalom Mbiling’i, amesema kuwa hadi sasa kila mwalimu nchini amewezeshwa kufundisha angalau somo moja la sayansi.

Dk. Mbiling’i amesema kuwa kiwango hicho kikubwa kilichofikiwa ni hatua muhimu katika kuboresha mchakato wa ufundishaji wa masomo ya sayansi. 

Ameongeza kuwa, mafanikio hayo yatasaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaosoma sayansi, kuongeza  ufaulu wa wanafunzi na kuandaa wataalam wengi ambao watasaidia kutatua changamoto mbalimbali  zinazoikumba jamii na watakuwa na uwezo  kushindana katika fursa za kitaifa na kimataifa.