Mkazi wa Mbezi Africana kortini tuhuma wizi Mita za DAWASA

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 02:15 PM Sep 24 2024
Mkazi wa Mbezi Africana kortini tuhuma wizi Mita za DAWASA

Emmanuel Kalungwana Mkazi wa Mbezi Africana, amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni kujibu shtaka la kuingilia miundombinu ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) ambalo ni kosa la Uhujumu Uchumi.

Kalungwana amefikishwa Mahakamani hapo na kusomewa shtaka lake na wakili wa Serikali, Salima Jafari mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Ramadhani Rugemalira.

Wakili wa Serikali alidai kuwa  mshtakiwa anadaiwa kuiba dira za maji (Mita 3) eneo la Wazo akiwa na lengo la kuziuza ili kujipatia fedha.

Mshtakiwa huyo anadaiwa kutenda kosa hilo tarehe 2 Agosti,2024.

Mshtakiwa baada ya kusomewa shtaka hilo amerudishwa mahabusu baada ya kushindwa masharti ya dhamana ambayo ni kiasi cha Shilingi laki tano (500,000) na wadhamini wawili.

Upande wa mashtaka umedai kuwa upelelezi bado haujakamilika. Baada ya kusomewa shtaka hilo, hakimu Rugemalila aliahirisha kesi hiyo hadi Novemba 2,2024.

Hata hivyo, kwa mujibu Sheria ya Maji Namba 5 ya mwaka 2019 Kifungu cha 61 kinaelekeza faini isiyopungua 500,000 na isiyozidi 50,000,000,au Kifungo kuanzia miaka miwili isiyozidi miaka mitano au vyote faini na kifungo kwa pamoja.