Washiriki 5,000 Tamasha la tatu la utamaduni fursa lukuki

By Joseph Mwendapole , Nipashe
Published at 04:30 PM Sep 17 2024
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro ameeleza kuwa, Tamasha la tatu la Utamaduni la Kitaifa Songea litatoa fursa lukuki kwa wakazi wa mkoa wa Ruvuma na mikoa ya jirani katika nyanja za kibiashara, bidhaa za asili, vyakula, malazi, usafiri na litaambatana na mafunzo, semina na midahalo mbalimbali kuhusu Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Ndumbaro amesema hayo katika Mkutano na Wanahabari Septemba 16, Manispaa ya Songea wakati anatambulisha Tamasha hilo litakalofanyika kuanzia Septamba 20 – 23, 2024 Uwanja wa Majimaji Songea.

Amesema tamasha hilo litahusisha maonesho ya ngoma na vyakula vya asili vya mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia tarehe 21 na 22, 2023. Kutakua na mashindano ya ngoma na vyakula hivyo na washindi watapata zawadi.

Kutakua na onesho Maalum la matumizi ya Kanga katika utamaduni wa mtanzania ikiwemo kanga inavyotumika kubeba watoto, kata kichwani, kujifunga pamoja na kutoa ujumbe, akielekeza pia kuwa kutakua na mbio fupi (Jogging) asubuhi ya tarehe 21, ambapo Vyama vya Jogging kutoka mikoa yote pamoja na Mkutano wa Vyama hivyo katika kukuza maendeleo ya Vyama hivyo.

Amesisitiza kuwa kilele cha tamasha hilo itakua ni Septemba 23, 2024 Uwanja wa Majimaji Songea na mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, amesema tamasha hilo mbali na burudani na Elimu, litaleta fursa za kiuchumi kwa Mkoa wa Songea zitaongezeka katika eneo la biashara, uwekezaji nankuitangaza Ruvuma Kimataifa, ambapo hadi sasa zaidi ya wananchi 5000 wamethibitisha kushiriki.

Tamasha hilo litatatunguliwa na Mdahalo wa Maadili Kitaifa, Semina ya Sensa na Maendeleo ya Sekta za Utamaduni Sanaa na Michezo, Mafunzo kwa wadau wa Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na Usiku wa burudani.