CRDB yajivunia kuvuka mipaka kimataifa kwa kuwekeza nje ya nchi

By Allan Isack , Nipashe
Published at 07:50 AM Sep 01 2024
MKURUGENZI Mtendaji wa Benki ya CRDB,Abdulmajid Nsekela

MKURUGENZI Mtendaji wa Benki ya CRDB,Abdulmajid Nsekela,amesema benki hiyo imefanikiwa kuvuka mipaka kimataifa kwa kuwekeza nje ya nchi kwa kuwa kabla ya kufanya uwekezaji huo,walifanya utafiti wa kutosha ambao ulisaidia benki kufanikiwa na kufikia malengo.

Alisema hayo jana jijini Arusha,wakati akitoa mada katika kikao kazi cha wenyeviti wa bodi na watendaji wakuu wa taasisi za Umma kinachoendelea kwa siku nne. 

Alisema baada ya kufanya utafiti wa kina wa sehemu walizokwenda kuwekeza imesaidia benki hiyo kufikia malengo ya kuvuka mipaka kwa kuwekeza nje ya Tanzania. 

Kadhalika alitaja sababu ya kwenda kuwekeza nje ya mipaka ,hasa katika nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa kuwa wana wateja wengi,pia nchi hizo zimekuwa zikifanya biashara na Tanzania. 

“Tunapokwenda kuwekeza kwenye soko la nje ni lazima kufanya utafiti wa kupata taarifa za kule unapotaka kuwekeza,fursa na kuanzia au kununua biashara ambayo utaingia ubia na wadau wa huko. 

“Unapokwenda kuwekeza huko, usiende kiujumla tafuta wadau utakaoingia nao ubia,kuwa na uongozi bora utakaokwenda sambamba na Serikali na teknolojia.alisema.alisema” 

Vilevile alisema uwekezaji walioufanya katika nchi ya Burundi ulikuwa ni rahisi kwa kuwa mtaji wa kuanzisha benki ni mdogo na huko kuna benki 15 tu. 

“Wakati tunaingia Burundi mwaka 2021 mtaji ulikuwa ni Dola za Kimarekani Milioni 13 na tuna fanya vizuri katika kapu la nchi hiyo na wamekuwa karibu na jamii na wadau wa maendeleo. 
“Tulichojifunza Burundi ukitaka kuwekeza ni lazima uwe na utulivu na kuielewa Serikali nini inachotaka na kuenda sambamba nayo.aliongeza.alisma” 

Wakati huko huko,alisema kuwekeza katika nchi ya DRC ni gharama kwa kuwa mtaji wa kuanzia benki ni Dolla za Kimarekani Milioni 50 wakati Tanzania ni Sh.bilioni 15. 

Pia alitaja changamoto ya kuwekeza katika nchi hizo, ni mitaji,sheria ni tofauti na zina kinzana,utofauti wa mila na desturi na lugha. 

Mkurugenzi huyo,alisema kuwa benki hiyo, wana mtaji wa Trilioni 1.9, mali (aseti) Trilioni 15,matawi 251,mawakala 21000 na wafanyakazi 400.

Kuhusu umiliki wa hisa,alisema kwa mtu mmoja mmoja wanamiliki hisa kwa asilimia 31,serikali wanamiliki asilimia 21,mashirika ya serikali asilimia 16 na vyama vya ushirika asilimia 6.8.

 Licha ya kuzungumza hayo,alisema benki hiyo, kwa mwaka 2019 walipata faida ya Sh.bilioni 120 na kwa mwaka 2023  faida ilikuwa ni sh.bilioni 423. 

Katika hatua nyingine, alisema CRDB itaanda mafunzo ya kuwajengea uwezo wakulima ili kuwapatia mikopo kupitia programu maalum,ambapo itawasaidia kujikwamua kiuchumi.

Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa (NEC), Stephen Wasira,ameitaka benki hiyo,kusaidia sekta ya kilimo nchini ikiwamo cha kutoa mikopo kwa wakulima kwenye kilimo cha umwagiliaji. 

“Mnawasaidiaje makampuni machana na vijana kwa kuwa hawana ajira na mikopo mara nyingi inatolewa kwa masharti magumu na wahitaji hawaipati kwa kutokukudhi vigezo, hivyo inakwenda kwa wenye uwezo na sio kwa walengwa,” alisema. 

Aidha Dk.Harrison Mwakyembe,alitumia fursa hiyo kuiomba benki hiyo,kupunguza riba ili vijana wengi waweze kukopa zaidi.