Mitungi 10,000 ya Taifa Gas yapokelewa Dodoma kumtua mama kuni kichwani

By Mwandishi Wetu , Nipashe Jumapili
Published at 12:32 PM Mar 10 2024
Meneja Mkuu wa Taifa Gas Tanzania Limited Devis Deogratius aki zungumza katika kongamano la wanawake kuhusu Nishati jijini Dodoma.
PICHA: MPIGAPICHA WETU
Meneja Mkuu wa Taifa Gas Tanzania Limited Devis Deogratius aki zungumza katika kongamano la wanawake kuhusu Nishati jijini Dodoma.

Kampuni ya Taifa Gas imekabidhi serikali mitungi elfu 10 ya gesi kama njia moja ya kuunga mkono kampeini ya Matumizi ya Nishati safi nchini.

Makamu wa Rais Dk. Phillip Mpango, aliyemuwakilisha Rais Mama Samia Suluhu Hassan, katika kongamano la wanawake la kuhimiza matumizi ya Nishati safi jijini Dodoma, alipokea Mitungi hiyo iliyokabidhiwa na Meneja Mkuu wa Taifa Gas Devis Deogratius. 

Akizumgumza katika kongamano hilo, Deogratius aliipongeza serikali kwa juhudi zake za kupambania watanzania ili wawe miongoni mwa nchi ambazo zinatamba duniani katika kutumia Nishati safi ya kupikia.

Katika kongamano hilo ambalo liliandaliwa na Wizara ya Nishati na kuhudhuriwa na mamia ya akina mama, kutoka pande zote za nchi, Deogratius alieleza mikakati kabambe ya Taifa gesi nchini inayolenga kuhakikisha gesi inapatikana katika kila mlango wa nyumba ya mtanzania.

Makamu wa Rais Dk.. Philip Mpango akipokea Mtungi wa Taifa Gas ikiwa ni miongoni mwa mitungi 10,000 iliyotolewa na kampuni hiyo.
Deogratius alisema Taifa Gas katika mikakati yake, itaendelea kufanya kazi na wadau wote wakiwemo serikali, kupitia wizara ya Nishati , wabunge , serikali za mikoa , wilaya na kadhalika ili kufanikisha agenda ya matumizi ya Nishati safi nchini. 

Makamu wa Rais Dk. Mpango alipongeza hatua hiyo ya taifa gas ya kutoa mitungi 10,000 na kusema itasaidia pakubwa katika kuhakikisha Makundi yanayostahili kupata gesi yanafikiwa na mitungi hiyo.

Hii ni mara ya pili ambapo Taifa gas inadhamini kongamano hilo la Nishati baada ya kongamano la mwaka 2022 lililofanyika jijini Dar es Salaam.