NSSF yaongeza wanachama wapya 291,266

By Shaban Njia , Nipashe
Published at 08:45 PM Oct 08 2024
 Meneja wa mfuko huo Aisha Nyemba
Picha:Mpigapicha Wetu
Meneja wa mfuko huo Aisha Nyemba

MFUKO wa Hifadhi ya Jamii(NSSF) Mkoa wa Kahama umefanikiwa kuongeza wanachama wapya 291,266 kwa mwaka 2023/2024 na sasa inajipanga kuendelea kutoa huduma bora na zenye tija kwa wateja wao.

Haya yamebainishwa na Meneja wa mfuko huo Aisha Nyemba wakati akifungua wikiya mteja kwa kuzungumza na kubadilisha mawazo na wanachama wao yenye kauli mbio"huduma bora muda wote".

Alisema, hadi kufikia mwishoni mwa mwaka wa fedha 2023/2024 mfuko ulikuwa na wanachama 1,354, 985 na waajiri 43,430 na mwaka huo pia ilipata wanachama wapya 291,266 huku malengo yao yalikuwa kuandikisha wanachama 324,321 kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Aidha alisema, mfuko umeboresha mfumo wa sekta isiyo rasmi mahususi kwa wanachama wote waliojiajiri, na umeandaa  skimu maalum kwa wafanyakazi walio katika sekta rasmi ili kuweza kuchangia kwa hiari kupitia skim hiyo.

Mkazi wa Ushetu William Mtambo aliwataka NSSF kuwatembelea wakulima mara kwa mara na kuwaelimisha umuhimu wa mfuko huo na mafao ya baadae ili kuwahamasisha kujiunga, wengi wanashindwa kuwa wanachama kwasababu ya kukosa elimu nasio vinginevyo.