Yanga yafunga usajili mpya, Pacome kuongezwa mkataba

By Adam Fungamwango , Nipashe
Published at 07:37 AM Jun 29 2024
Rais wa Klabu hiyo, Hersi Said.
Picha: Maktaba
Rais wa Klabu hiyo, Hersi Said.

WAKATI uongozi wa klabu ya Yanga ukijiandaa kumuongezea mkataba kiungo mshambuliaji wake Pacome Zouzoua, umetangaza kukamilisha na kufunga usajili wake msimu huu na sasa wanasubiri kuwatangaza rasmi wachezaji wote waliowasajili.

Rais wa Klabu hiyo, Hersi Said amesema jana kuwa tayari wameshamaliza usajili na sasa vimebaki vitu vichache ikiwemo Idara ya Habari kuweka utaratibu ili waanze kuwaweka hadharani.

"Tupo makini, kazi kubwa tumeshaifanya, tumeshasajili na karibuni asilima 99 kazi imekwisha, hivi sasa tumeiachia tu Idara ya Habari kutengeneza njia nzuri ya kutambulisha wachezaji wote tuliowasajili," alisema Hersi.

Alisema katika usajili wao wamejikita tu kwenye maeneo ambayo wanaona yana mapungufu na si vinginevyo.

"Suala la usajili huu ndiyo wakati wake na ni muhimu sana kuliko wakati mwingine wowote, ni kipindi cha kutuliza akili ili kupata wachezaji wazuri.

Sisi Yanga kuna maeneo ambayo tumelazimika kuyaboresha kwenye kikosi chetu ili kuwa bora zaidi, kwa hiyo nichukue fursa hii kuwaambia wana Yanga wawe tayari kuanzia tarehe moja Julai tutaanza kuelezea, au kutoa taarifa za usajili za wachezaji wetu wapya, wale tunaowaongezea mikataba na tutakaowaacha," alisema Hersi.

Wachezaji wanaohusishwa kutua kwenye klabu hiyo ni Wakongomani watatu, beki wa kushoto, Chadrack Boka kutoka FC Lupopo, kiungo mkabaji, Agee Basiala wa klabu ya Maniema Union na winga Emmanuel Lobota anayeichezea Singida Black Stars.

Mchezaji mwingine anayetajwa ni Chikamso Okechukwu, beki wa kati kutoka klabu ya Enyimba.

Wakati huo huo, klabu hiyo imesema ipo kwenye mazungumzo ya kumuongeza mkataba kiungo mshambuliaji, Pacome raia wa Ivory Coast ambaye kwa siku za karibuni amekuwa akihusishwa kutimkia klabu za FAR Rabat ya Morocco na Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini.

Ingawa Pacome ana mkataba wa mwaka mmoja zaidi  wameamua kukaa naye ili wampe mkataba mwingine ili kuhakikisha anasalia kwa muda mrefu ndani ya timu hiyo.