KUMBUKIZI YA NYERERE: Viongozi na wananchi jipekueni ni wazalendo mnaishi kanuni zake, vipi tamaa ya mali, ubadhirifu

By Rahma Suleiman , Nipashe
Published at 09:52 AM Oct 15 2024
Baba wa Taifa Mwalimu Julius  Nyerere
Picha;Maktaba
Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere

NI miaka 25 tokea Tanzania lilipompoteza mwasisi wake Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Oktoba 14, 1999 akiwa kwenye matibabu kwenye Hospitali ya Mtakatifu Thomas huko Uingereza.

Alipotwaliwa wapo baadhi ya watu walisema   huenda  Tanzania inekumbwa na hali ya kutokuelewana  na kuvutana katika baadhi  ya mambo  na hata  wananchi kugawanyika.

 Hilo halijawezekana kwani baada ya miongo miwili na nusu sasa  hakujawa japo hata na ishara ya kutokea mpasuko wa kitaifa au mgawanyiko, badala  yake Tanzania  imezidi kuwa moja na kupata  mafanikio makubwa kisiasa, kiuchumi na kijamii.

 Pamoja na kwamba  miaka 23 ya utawala wa Mwalimu  Nyerere  taifa lilikuwa  likifuata mfumo wa chama kimoja, hata pale viliporuhusiwa vyama vingi, nchi imebaki katika mshikamano.

 Kwanini basi hakujawa na mgawanyiko, mpasuko au utengano wowote? Hakuwezi kutokea na yote hayo  kwa kuwa waasisi wa taifa hili,  Mwalimu  Nyerere na mwenzake Sheikh  Abeid  Amani Karume, waliweka misingi, miiko, uadilifu na kanuni  za kudumisha mtangamano.

 Ndiyo  maana hata alipoingia madarakani  Rais  wa Awamu ya Pili, Mzee Ali  Hassan Mwinyi, taifa  limeendelea kubaki vilevile bila kutikisika au kushtushwa na lolote.

Licha ya waasisi hao kuondoka duniani wakiacha nchi ikiwa moja, yenye katiba zake, kanuni, taratibu, miiko na miongozo kama nguzo na kinga zinazolinda usalama wa taifa, watu na utamaduni mmoja.

 Nyerere ambaye amekufa miaka 25 iliyopita ameiacha Tanzania ikishikamana bila ukabila, udini, ukanda wala ubaguzi wa ina yoyote.

 Amewaacha Watanzaia wakiitana  ndugu. Kila mmoja akiheshimu ubinadanu na utu wa mwenzake, kuthamini  heshima ya kila mmoja, kusaidiana na kuhurumiana. Watanzania hawajivunii dini, kabila wala rangi zao.

 Katika muda wote wa miaka  ya uongozi wake, Mwalimu Nyerere alisimamia misingi ya uongozi na kuwataka viongozi katika nafasi  zao  kutambua kuwa binadamu wote ni sawa.

 Alikuwa akisema mara kwa mara katika maisha ya uongozi wake wakati wa kupigania uhuru na hata baada ya kujitawala kuwa, kila mmoja anastahili kuheshimu wenzake na kuheshimiwa pia, akithamaniwa na kutambuliwa utu wake.

Nyerere hakuwa mtetezi wa haki za binadamu kwa Tanzania peke yake bali akipaza sauti yake kimataifa. Kila mahali duniani ambako binadamu walibaguliwa na kutengwa, Mwalimu  hakusita kuwasemea.

 Wakati Tanzania kila mwaka wamekuwa wakimkumbuka mwasisi wao, duniani kwenye midahalo na mijadala mbalimbali, kiongozi  huyo hukumbukwa kwa uongozi  wake bora uliosifika hasa usiothamani mali na utajiri.

 Nyerere na mshirika mwenzake Karume ndio  waliokuja na wazo la kuyaunganisha mataifa ya Tanganyika na Zanzibar  mwaka 1964 na kuundwa kwa taifa ambalo halikuachwa na wakoloni liitwalo Tanzania.

 Mwalimu Nyerere hakuishia hapo lakini pia alihakikisha mataifa yote ya kusini mwa Afrika yaliokuwa yakitawaliwa kibabe na wakoloni nayo yanajikomboa na kujitawala.

 Akaweka mkazo mkubwa wa kuhifadhi vyama vya ukombozi kwenye ardhi ya Tanzania, wapigania uhuru wake hadi pale walipopata uhuru katika nchi zao.

 Kiongozi  huyo ndiye aliyeweka mkazo na kuhakikisha inaundwa Jumuiya  ya Afrika Mashariki  mwaka 1967 kati ya Tanzania, Kenya na Uganda ingawa  baadhi  ya viongozi wenzake hawakutaka mpango huo.

 Zikazuka fitna, mizengwe na kila aina ya hila zilizotaka jumuiya hiyo ife. Kweli ikafa miaka 1977 na mataifa wanachama wakarudi nyuma kimaendeleo baada ya mafanikio makubwa waliyoyapata kupitia mtangamano.

 Hata hivyo  baada ya kupuuza mawazo ya Nyerere, viongozi  walikuja kuongoza madola  baadaye mwaka 1999 wakaanzisha tena mchakato  wa kuunda Jumuiya ya Afrika Mashariki kama alivyotaka Nyerere miaka mingi iliyopita safari hii ikiwa na mataifa mengi zaidi.

 Mbali na Kenya, Uganda  na Tanzania imezileta pamoja Rwanda, Burundi, Congo, Sudan Kusini na Somalia.  

Nyerere ametwaliwa, hatunaye tena, hatarudi lakini fikra zake, maono na mawazo  yake,  yataendelezwa kwa bidii  na kila  rais au utawala  utakaoshika madaraka kwakuwa taifa hili lina misingi, asili na miiko ambayo ilianzishwa na waasisi hasa yeye na Karume.

Mwalimu  alichukia  unyonyaji, uonevu, kukandamiza haki za wanyonge, unyanyasaji lakini pia hakuwa kiongozi  aliyependa upendeleo.Akichukia rushwa, ubadhirifu wa  mali  za umma na matumizi mabaya ya rasilimali za taifa.

 Kiongozi  huyo atakumbukwa kwa uongozi  wake ambao hakuonyesha hata mara moja anahamanika na kutaka utajiri, hakuwa mkwapuzi wa mali za umma wala  kujilimbikizia mali kama ilivyokuwa kwa baadhi ya  viongozi.

 Mwalimu Nyerere  akiamini katika nadharia ya uongozi si ajira inayohitaji malipo lakini pia aliamini kila binadamu yuko huru kuchagua anachokiamini alimradi jambo  hilo halivunji sheria za nchi wala  katiba.

 Taifa linapokikumbuka kifo chake, lazima viongozi wajipekue, Watanzania pia wajichunguze endapo bado wanaishi  katika ndoto zake hizo au wameziacha kanuni hizo na sasa wanakwenda segemnege, shaghalabaghala au  ndivyo sivyo.