IAA kufungua kampasi mpya mbili nje ya nchi

By Grace Mwakalinga , Nipashe
Published at 05:01 PM Dec 10 2024
Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Eliamani Sedoyeka
Picha:Mpigapicha Wetu
Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Eliamani Sedoyeka

CHUO cha Uhasibu Arusha (IAA), kimetangaza mpango wa kufungua kampasi mpya nje ya nchi, moja katika Visiwa vya Comoro na nyingine Sudan Kusini , kufuatia mahitaji makubwa ya elimu ya juu na fursa za maendeleo katika maeneo hayo.

Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Eliamani Sedoyeka, ameeleza mpango huo, wakati wa kikao  na wahariri wa vyombo vya habari kilichofanyika leo katika ukumbi wa chuo hicho jijini Arusha.

Profesa Sedoyeka amesema kuwa, hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kukifanya chuo hicho kuwa taasisi ya kimataifa inayotoa huduma bora za elimu kwa kukidhi viwango vya kitaifa na kimataifa.

Amesema  wamelenga kukimataifisha chuo hicho kwa kigezo cha kuandaa mitaala inayoendana na soko la ndani na nje ya nchi, teknolojia za kufundishia, kujifunzia  kwa njia ya mitandao.

"Mpango huu unalenga kuboresha upatikanaji wa elimu ya juu na kuimarisha nafasi ya IAA katika kutoa mchango wa kielimu ndani na nje ya mipaka ya Tanzania," tumejipima tunakidhi vigezo vya kufanya hivyo,” amesema Profesa Sedoyeka.

1

Amesema IAA, kimejipambanua kwa ubora katika mafunzo ya uhasibu, biashara,  tehama,  fedha , utalii na ukarimu kulingana na mahitaji ya soko  na  kufungua kampasi mpya kwenye mikoa ya Dodoma, Manyara na Ruvuma  ili  kuongeza wigo wa huduma zake.

Prof. Sedoyeka, amesema kwa sasa chuo kina watumishi 370, kati yao 32 ni wenye Shahada  ya Uzamivu na wanatarajiwa kufikia 100 baada ya wengine 88 kumaliza masomo yao.

Ameongeza kuwa mwaka 2025, chuo hicho kinatarajiwa kuwa na  wanafunzi 20,000 idadi ambayo itakifanya kuwa miongoni mwa vyuo vikuu vyenye idadi kubwa ya wanafunzi nchini.
2