Chalamila atangaza kiama kwa waganga wanaosababisha mauaji

By Sabato Kasika , Nipashe
Published at 04:39 PM Jun 20 2024
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk.Amon Mpanju kulia akiwa na viongozi wengine katika maadhimisho hayo.
Picha: Sabato Kasika
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk.Amon Mpanju kulia akiwa na viongozi wengine katika maadhimisho hayo.

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ametangaza kuanzisha operesheni Maalum ya kuwasaka waganga wote wa kienyeji ambao wanajihusha na vitendo vinavyochangia kuwapo mauaji ya watu wenye ulemavu.

Chalamila ameyasema hayo katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Afrika ambayo kimkoa yalifanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam jana.

Amesema, maadhimisho hayo yaliandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, huku Chalamila akiwa mgeni rasmi kwa niaba ya Waziri Dk.Dotothy Gwajima.

Amesema, ataandaa utaratibu maalum wa kufanya operesheni hiyo baada ya kukutana na viongozi wenzake.

Mkuu huyo wa mkoa amesema,  kama waganga wa aina hiyo wapo mkoani mwake, wajiandae kuhamia kwingine, kwa kuwa hawataki mkoani mwake.

Baadhi ya washiriki wa maadhimisho hayo.

"Wanashawishi watu kuua wenye ulemavu wa ngozi, lakini pia wanaweza kusema  wanatamka watu wafupi, wenye vipara au vyovyote vile. Sasa natangaza kuanza msako," alisema Chalamila.

Aidha, amekemea watu kushabikia vitendo vya udhaliliaji wa watoto na utu wao, wazazi kuwa na matendo mema ambayo watoto wanaweza kujifunza kwao.

"Tusilalamikie teknolojia kuwa inamomonyoa maadili, wawawekee watoto wao kiwango ya kutumia teknolojia badala yake tunawasaidie kujua umuhimu wake na jinsi ya kutumia," amesema..
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk. Amon Mapanju, amesema kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu haina budi kuzingatiwa na wazazi na walezi.

Baadhi ya wanafunzi wakiwa katika maadhimisho hayo.

Ameitaja kaulimbiu hiyo kuwa ni;  "Elimu Jumuishi kwa Watoto Kuzingatie Ujuzi, Maadili na Stadi za Kazi; Wajibu wa Wazazi na Jamii Katika Kumsaidia Mtoto katika Kufikia Malengo yake kwa Maendeleo ya Baadaye".

"Lengo la kaulimniu hii  inakumbusha kupaza sauti kwa watoto na kuhakikisha wanapata elimu inayoendana na sayansi na teknlojia itakayowawezesha kwenda sambamba na soko la ajira kwa kuajiriwa au kujiajiri na kutumia vifaa vya teknolojia ikiwamo kompyuta, hivyo ni muhimu wazazi na walezi kuharakisha watoto wao wanapata elimu," amesema Dk. Mapanju.

Mkuu wa Dar es Salaam, Albert Chalamila (wa tano kutoka kushoto waliokaa), baada kumaliza kuhutubia katika maadhimisho hayo.