Jali, moshi huu wa injini unaua

By Tuntule Swebe , Nipashe
Published at 11:21 AM Jun 18 2024
Mbongambonga.
Picha: Mtandao
Mbongambonga.

SUMU na taka za sumu zinazotoka kwenye injini si salama, zina karbon au hewa ukaa inayoweza kukuua, kuchafua hewa na chakula au bidhaa.

Ndiyo maana wataalamu wa  afya wanasema kufanya  kazi, kula vyakula vilivyochafuliwa au kukaa karibu na moshi ambao una gesi hizo kwa kiasi kikubwa ni hatari kwa yeyote.

Ikumbukwe kemikali na hewa hii  hutoka wakati injini zinazotumia petroli au dizeli  zinapopumua na moshi huo kusambaa angani na pembeni.

Huwafikia  walioko pembeni mwa barabara  na kusababisha kupata madhara yanayojificha  lakini yanayoweza kuibuka baada ya miaka kadhaa.  

Baada ya miaka mingi au muda mrefu magonjwa  yanayotokana na hewa chafu huanza kuonekana, kuanzia  machoni, kifuani, kwenye ngozi na kooni  kote yakisababisha athari.

Kwa kawaida moshi huo huumiza  macho, pua na koo na harufu yake inaweza kusababisha kichefuchefu lakini wengi huchukulia kuwa ni kitu cha muda mfupi.

Uchunguzi wa kiafya unaonyesha kwamba baadhi ya watu waliovuta  moshi mzito wana matatizo kwenye mapafu yanayosababisha  kupumua kwa shida, mafua, kukohoa mara kwa mara  na kuwa na mzio au aleji.

 Kuzoea kuvuta moshi huu  kunaweza kusababisha athari za haraka kama kuwashwa machoni, puani na koo kukereketwa na hata mafua.

Inaelezwa na wataalamu kuwa moshi wa injini za  magari, pamoja na bajaji  na pikipiki unaweza kuleta madhara makubwa kama  kwa afya watu na mimea hasa iliyo kando ya barabara.

Lakini, inavyoelekea wengi hawalielewi tatizo hilo na wala hawachukui tahadhari, mfano wafanyabiashara za vyakula karibu na barabara wana hatarisha maisha yao na wateja wao pia.

Kwa mfano, wale wanaouza vyakula  mfano pweza, kachori, mishkaki, chipsi na  vitafunwa kwenye stendi za mabasi mijini au kwenye barabara vinachafuliwa na vumbi pamoja na moshi wa vyombo vya moto.

Ni vyema wajue kuwa hula na kuishi kwenye kemikali za simu inayotoka kwenye injini.

Wanaokula na wanaotayarisha huweza kuugua magonjwa kama kuharisha, kutapika, kuhara damu, tumbo kujaa gesi, kupata kichefuchefu na kukosa hamu ya kula.

Ni vyema kukawa na udhibiti wa biashara ikiwamo kuuza vyakula karibu na barabara au vituo vya mabasi ambako magari hupumua. Aidha hata kukataza  kupanda mboga barabarani ambazo huchafuliwa na moshi wa injini.

Wafanyabiashara wa vyakula, matunda, wakulima wa mboga na matunda pembeni ya barabara na wauza  mboga hizo pembezoni wajiepusha na hatari hizo za kiafya.

Jamii nayo inahitaji elimu na kupewa ufahamu kuhusu madhara ya kula vyakula vilivyochafuka na sumu hasa za kemikali za moshi wa injini ili kujiepusha na magonjwa.

Bila shaka wafanyabiashara, wakulima kila mmoja  kwa pomoja wanatakiwa kuwa na tahadhari  kwani magonjwa ni sababu ya kuyumba kwa maendeleo kwenye  ngazi za familia, jamii na taifa pia.

Visingizio kuwa wanatafuta fedha za kujikimu ndiyo maana wanalima au kuuza bidhaa za vyakula zilizochafuliwa na moshi wa injini kisikubalike kwani vyote vinadhuru afya.

Ni vema kufikiri kuwa  hata usipoathirika leo kwa kupata magonjwa yanayoambatana na moshi huo hapo baaadaye kuna  hatari ya kusumbuliwa na maradhi  kwani mtu anapokua na umri mkubwa matatizo ya kiafya yaliyojificha kwa muda mrefu  huibuka.

Ikumbukwe kuwa ni bora kuchukua tahadhari kwani kadiri watu wanavyozeeka, mifumo ya kinga hudhoofika vilevile, uzee una uwezekano mkubwa wa kuwa na changamoto za kiafya kuliko ujana.

 Ni muhimu kuwa na tahadhari na umakini kwa kuukwepa moshi wa  petroli na dizeli na kuacha kufanya biashara karibu na barabara ili kujikinga na magonjwa ambayo yanaweza kuepukika hasa kutoka kwenye vyombo vya moto.