"Tuunge mkono jitihada za Dk.Samia katika Nishati Safi ya Kupikia"- Kapinga

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 10:59 AM Sep 08 2024
Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga.

Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga amewataka wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan katika matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Kapinga  ameyasema hayo leo Septemba 08, 2024 jijini Dar es Salaam wakati wa Tamasha la AZIMIO LA KIZIMKAZI  ambalo limetumika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia likihusisha  Mamalishe na Babalishe Jijini Dar es Salaam. 

"Kiongozi aina ya Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye ana maono ya nishati safi ya kupikia hapatikani mara zote, hatokei mara zote hivyo tuna wajibu wa kumuunga mkono katika ajenda hii ambayo faida zake ni nyingi kiafya, kimazingira, kiuchumi na kijamii." amesema Kapinga
 
Ameongeza kuwa,  Rais Samia amesimamia maono yake na kuwafanya Watanzania, Afrika na Duniani kote kusimama pamoja naye katika matumizi ya nishati safi ya kupikia. 

Ameeleza kuwa, Rais Dk. Samia anathamini watanzania wote bila kujali hali zao na ndio maana ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia inagusa makundi yote ya Wananchi hivyo nao wana wajibu kumuunga mkono katika kuiletea Tanzania maendeleo.