Raia wa China aliyejifungua mapacha watatu Dar ashukuru kwa huduma nzuri

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 04:46 PM Aug 27 2024
Raia wa China aliyejifungua mapacha watatu Dar ashukuru kwa huduma nzuri.

RAIA wa China, Liya Zhang (31), ambaye amejifungua watoto mapacha watatu wa kiume katika hospitali ya Regency ya jijini Dar es Salaam ameshukuru kwa huduma nzuri alizopata.

Raia huyo alijifungua watoto hao siku ya Jumapili usiku hospitalini hapo na mpaka sasa anaendelea vizuri yeye na watoto wake hao watatu.

Akizungumza hospitalini hapo, Liya alisema awali wakati anahudhuria kliniki alidhani kuwa ana ujauzito wa mtoto mmoja lakini baada ya vipimo alishtuka kuambiwa kuwa  ana watoto wa tatu.

“Nawashukuru sana madaktari bingwa wa watoto, Dk. Rahim na Dk. Supriya Khan kwa namna walivyonihudumia tangu awali mpaka najifungua, nimepata huduma nzuri sana hapa Regency na watoto wangu kama unavyowaona wako vizuri kabisa,” alisema Liya kwa lugha ya Kiswahili fasaha.

Liya alisema si mara yake ya kwanza kujifungua hospitalini hapo kwani mwaka 2009 alijifungua mtoto wa kwanza wa kike hospitalini hapo na baadaye alikuja kujifungua mengine wawili wa kiume pia hospitaini hapo hapo na sasa amefurahi kupata watoto wa kiume watatu.

“Nilipata mtoto mmoja wa kike mwaka 2009 na baadaye nikapata  mapacha wawili wa kiume na juzi Jumapili nimepata mapacha watatu kwa hiyo sasa nina jumla ya watoto sita na wote nimejifungua katika hospitali hii hii ya Regency na nadhani nitakuwa nimemaliza kwa kweli inatosha,” alisema Liya huku akicheka kwa nguvu.

Daktari bingwa wa watoto wa Regency, Dk. Rahim alisema wamekuwa wakimhudumia Liya tangu uzao wake wa kwanza ambapo alipata mtoto wakike hospitalini hapo na ujauzito wa pili ambapo alifanikiwa kupata watoto wa kiume mapacha.

“Na huu ni ujauzito wake wa mara ya tatu ambapo amefanikiwa kupata mapacha watatu wote wa kiume na uziri ni kwamba anaimani nasisi kwa muda mrefu kwani kila anapotaka kujifungua amekuwa akija hapa Regency na tunashukuru watoto wake wote wanaendelea vizuri sana,” alisema

“Tumekuwa tukihudumia wanawake wengi sana wanaojifungua lakini hii ni mara ya kwanza hapa Regency kuhudumia mwanamke kupata watoto watatu, hii ni habari njema kwetu sote,” alisema