Kapinga: Serikali inaendelea na majadiliano na kampuni za nishati za kimataifa

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 06:24 PM Aug 29 2024
Naibu Waziri wa Nishati,Judith Kapinga

Naibu Waziri wa Nishati,Judith Kapinga amesema Serikali inaendelea na majadiliano na Kampuni za Nishati za Kimataifa (International Energy Companies - IEC’s) kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi asilia kuwa Kimiminika – LNG na yakikamilika Serikali itaupeleka kwenye hatua inayofuata.

Kapinga amesema hayo leo Agosti 29, 2024 bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Joseph Khenani aliyetaka  kufahamu lini Serikali  itapeleka bungeni mkataba kati ya Tanzania na Wawekezaji wa Gesi asilia wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 70 kwa ajili ya kujadiliwa.

"Mradi huu unamanufaa makubwa sana kwa Taifa letu, majadiliano haya ni muhimu kwa sababu ndio yanayoweka msingi wa kodi, mirabaha pamoja na ulinzi wa vigezo wa Nchi kunufaika kiuchumi", amefaganua Kapinga. 

Amelihakikishia bunge kuwa suala la mradi wa LNG ni kipaumbele katika Serikali na majadiliano yanaendelea na yapo katika hatua nzuri.

Kuhusu kuagiza gesi ya LPG kwa mfumo wa uagizaji wa pamoja ili kuleta unafuu wa bei kwenye gesi, Kapinga amesema Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) wanahakikisha soko la gesi linakuwa himilivu ili kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa kwa urahisi.

Naibu Waziri wa Nishati,Judith Kapinga .