Wanawake waomba unyenyekevu wahudumu wodi ya wazazi

By Julieth Mkireri , Nipashe
Published at 04:52 PM Feb 20 2025
Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, Dk. Abdulkadir Sultani.
Picha: Mpigapicha Wetu
Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, Dk. Abdulkadir Sultani.

Baadhi ya wanawake waliopata huduma ya kujifungua katika Kituo cha Afya Mkoani, Kibaha, wamepongeza huduma bora zinazotolewa huku wakiomba wahudumu wengine kwenye wodi ya wazazi kuwa wanyenyekevu zaidi ili kuondoa malalamiko kwa serikali.

 Wanawake hao wamesema kuwa unyenyekevu wa madaktari na wauguzi katika kituo hicho umevutia wengi kutoka maeneo mbalimbali, hata nje ya Mkoa wa Pwani.

Amina Rashid, mkazi wa Kiluvya, Dar es Salaam, amesema aliamua kujifungulia katika kituo hicho licha ya kuwepo vituo vya afya karibu naye kutokana na huduma bora anazosikia kutoka kwa waliowahi kutibiwa hapo.

"Nilikuja hapa kwa sababu madaktari na wauguzi wanawahudumia wagonjwa kwa heshima na kuwashauri vizuri," amesema Amina.

Naye Honorina Denis, mkazi wa Kibamba, amesema alichagua kituo hicho baada ya kupata ushuhuda mzuri kutoka kwa ndugu yake, hali iliyomfanya kuacha vituo vingine na kuhamia huko kwa huduma ya kujifungua.

Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, Dk. Abdulkadir Sultani, amesema kituo hicho kilichoanzishwa kama zahanati mwaka 1983, kilipandishwa hadhi kuwa kituo cha afya mwaka 2015.

Tangu mwaka huo, idadi ya wanawake wanaojifungua imeongezeka kwa kasi.

  • Mwaka 2015-2017, kituo kilihudumia wanawake 250 hadi 350 kwa mwezi, na kwa siku wanawake 8-10 walikuwa wakijifungua.
  • Baada ya maboresho, kituo kinahudumia wanawake 300 hadi 400 kwa mwezi, huku jengo lake likiwa na uwezo wa kupokea wanawake 10-12 kwa siku.
  • Kwa sasa, kutokana na uhitaji mkubwa, idadi hiyo imepanda hadi wanawake 450 hadi 600 kwa mwezi, ambapo asilimia 50 wanatoka Dar es Salaam katika maeneo ya Kibamba, Kiluvya, Ubungo, Kimara, Goba na Mbezi.

Chati inayoonyesha mwenendo wa ongezeko la wajawazito wanaojifungua katika Kituo cha Afya Mkoani Kibaha kwa kipindi tofauti.
Dk. Abdulkadir amesema wanawake wengi wanaotoka nje ya Kibaha hutumia kituo hicho kwa ajili ya kujifungua, licha ya kuhudhuria kliniki katika maeneo yao.

“Tunajitahidi kutoa huduma bora na tunawaahidi wanawake wote kuwa tutazidi kuboresha huduma zetu,” amesema.

1