Serikali kujenga kituo kipya cha afya Mahuninga

By Mwandishi Wetu , Nipashe Jumapili
Published at 04:43 PM Oct 20 2024
Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) William Lukuvi.
Picha:Mpigapicha Wetu
Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) William Lukuvi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) William Lukuvi ambaye pia ni Mbunge wa Isimani amesema Serikali kupitia Benki ya Dunia imetoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Mahuninga.

Ametoa Kauli hiyo wakati wa ziara yake kukagua miradi ya maendeleo katika Jimbo la Isimani lilopo mkoani Iringa jana ambapo amefanya mkutano katika vijiji vya Kisilwa Mahuninga na Makifu vilivyopo katika kata ya Mahuninga.


Alifafanua kwamba Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuimarisha huduma za afya; huduma za elimu, huduma za maji; ujenzi wa miundo mbinu ya umwagiliaji, ujenzi wa miundo mbinu ya barabara na hivyo wananchi wanapaswa kuendelea kuweka nguvu katika jitihada za kuchochea maendeleo ili kuimarisha uchumi.

Waziri lukuvi alisema, “Ujenzi wa kitu hicho cha afya utajumuisha ujenzi wa majengo manane mapya, ikijumuisha jengo la wagonjwa wa nje, jengo la maabara, jengo la kinamama na mtoto, jengo la kuhifadhi maiti, jengo la mionzi, jengo la kufulia, jengo la upasuaji na fedha za ujenzi imeshawekwa kwenye akaunti ya Mahuninga.” alisema na kuongeza kuwa;


"Namshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia kwa kutujali sana wanaisimani, tumepata fedha nyingi ndani ya kipindi cha miaka mitatu, ambazo zimeleta mabadiliko makubwa ya kimaendeleo katika Jimbo la Isimani." alisema 


Katika hatua nyingine Waziri Lukuvi, alitoa rai kwa wananchi wenye sifa za kujiandikisha kujitokeza kujiandikisha kwa ajili ya kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa bila kujali itikadi za vyama ili kujenga msingi mzuri wa kuchagua viongozi.

“tunaamini mwakani tutafanya vizuri zaidi katika uchaguzi wa Madiwani wabunge na Rais,” alisema 

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Mahuninga, Benitho Kisogole alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi kugharamia miradi ya Maendeleo.

“Ujenzi wa Miundo mbinu ya elimu kwa kipindi cha mwaka 2023-2024 umesaidia sana kuboresha mazingira kufundisha  hasa katika  ujenzi wa vyumba vya madarasa, vyoo na mabweni hivyo ni wajibu wetu kushirikiana ili ujenzi uishe kwa wakati,” alisema