WCF ipo kulinda nguvu kazi: Dk. Mduma

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 10:36 PM Jul 04 2024
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dk. John Mduma.
Picha: Mpigapicha Wetu
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dk. John Mduma.

MKURUGENZI Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dk. John Mduma, amewahakikishia waajiri na wafanyakazi kuwa Mfuko huo upo kwa ajili ya kulinda nguvu kazi na hivyo kuunga mkono juhudi za serikali katika kuhamasisha biashara na uwekezaji nchini.

Dk. Mduma ameyasema hayo Leo Julai 4, 2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye banda la Mfuko huo katika Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam, yanayoendelea kwenye viwanja vya Julius Nyerere, maarufu viwanja vya Sabasaba.

Alisema WCF inashiriki katika Maonesho hayo kwa lengo kukutana na wadau ili kutoa elimu kuhusu shughuli zitolewazo na Mfuko.

“Kama ambavyo kaulimbiu ya Maonesho haya inavyosema “Tanzania Sehemu Sahihi kwa Biashara na Uwekezaji”, WCF tunwahakikishia wawekezaji tupo kwa ajili ya kulinda nguvu kazi kwa kulipa fidia pindi Mfanyakazi anapopatwa na madhila ya kuumia au kuugua wakati akitekelza majukumu yake kwa  mujibu wa sheria na endapo atapoteza maisha basi wategemezi watalipwa fidia, amefafanua Dk. Mduma.