Wampongeza Rais Samia kuokoa maisha ya watoto njiti

By Frank Monyo , Nipashe
Published at 09:44 PM May 07 2024
Muuguzi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya akiwa na akinamama waliojifungua watoto njiti.

Kwa muda mrefu kinamama waliokuwa wanajifungua watoto kabla ya wakati (njiti) wamekuwa wakipatwa na hofu na mashaka kuhusu mustakabali wa maisha ya watoto wao kwakuwa inaelezwa wengi wa watoto hao walikuwa wakipoteza maisha kutokana na kukosa huduma bora za uangalizi kwa mama na mtoto.

Hata hivyo jambo hilo kwa sasa linaonekana kuwa historia kutokana na maboresho ya mifumo ya kitaalamu na uwepo wa Madaktari Bingwa wabobezi kwenye Hospitali mbalimbali za umma hapa nchini ambapo uangalizi dhidi ya watoto hao umekuwa ukifanywa kitaalamu zaidi.

Hilda Msigwa, Mkazi wa Mkoa wa Songwe na Rose Masebo, Mkazi wa Mtaa wa Mabatini Mbeya ni miongoni mwa kinamama mashuhuda, ambapo wawili hao kwa sasa wamelazwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya wakipatiwa uangalizi maalumu wa huduma ya Kangaroo baada ya kujifungua watoto wao kabla ya wakati (njiti).

Katika maelezo yao wamesema kuwa watoto wao wamezaliwa wakiwa na gramu tano (5) ndani ya kipindi cha miezi miwili (2) pekee watoto hao wamefikisha kg 1.5 jambo ambalo limewapa faraja kubwa.

Wametumia nafasi hiyo kutoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan kwa namna alivyofanikisha mageuzi makubwa kwenye sekta ya afya nchini ambayo yameokoa maisha ya watoto wengi waliozaliwa kabla ya wakati (njiti).