Makonda: Rais Samia anataka wananchi wa Arusha kunufaika na utalii

By Beatrice Shayo , Nipashe
Published at 03:46 PM Apr 30 2024
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul  Makonda.
Picha: Mpigapicha Wetu
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda amesema dhamira ya Rais, Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kila mwananchi wa Arusha ananufaika na sekta ya Utalii.

Makonda ameyasema hayo leo wakati wa kongamano la uwekezaji kwenye sekta ya utalii lililofanyika mkoani Arusha.

 Amesema kongamano hilo zipo jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali ili kuweka mazingira mazuri ya wananchi kunufaika na fursa ya utalii mkoani Arusha.

Amesema serikali yake ya mkoa imewekeza nguvu kubwa zaidi katika suala la ulinzi na usalama ili kuhakikisha wageni na watalii wanaifurahia Arusha na kutoa fursa kwa wawekezaji na wafanyabiashara kufanya shughuli zao kwa uhuru zaidi.

Aidha, amesema hatua ambazo amezichukua katika kutimiza maelekezo ya Rais Samia  katika kukuza utalii mkoani Arusha tayari  wameanza kufunga kamera za ulinzi na taa za barabarani kwenye maeneo mbalimbali ya mkoa.

Amesema ifikapo Julai mwaka huu mkoa wa Arusha anataka uwe unaoongoza kwa kuwa na kamera na Taa nyingi kuliko mkoa mwingine wa Tanzania.

Makonda ametumia fursa hiyo kuiomba serikali kufanya marekebisho ya barabara za mkoani Arusha kutokana na ubovu mkubwa kwenye barabara za katikati ya Jiji na barabara za kuingia kwenye Mbuga na hifadhi zilizopo pembezoni mwa mkoa huo.