Kijana matatani kwa kutaka kujiua

By Vitus Audax , Nipashe
Published at 01:10 PM May 08 2024
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Wilibroad Mutafungwa.
Picha: Maktaba
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Wilibroad Mutafungwa.

JESHI la Polisi Mkoa wa Mwanza linatarajia kumhoji Mwikwabe Range (20) kwa tuhuma za kutaka kujiua kwa kujirusha kwenye daraja la watembea kwa miguu lililopo eneo la Mabatini kwa kinachodaiwa ni kutokana na wivu wa mapenzi.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Wilibroad Mutafungwa amesema kuwa hatua hiyo inafuatia mtuhumiwa huyo kuonekana katika picha ya video iliyosambaa juzi katika mitandao ya kijamii.

Kipande cha picha hiyo kilimuonyesha mtuhumiwa huyo akijirusha katika daraja hilo kwa kile kilichoelezwa kukerwa na kitendo cha mpenzi wake aliyekuwa akimsomesha kugundua kuwa amezaa na mwanamume mwingine.

Mutafungwa, amesema mtuhumiwa huyo, Mkazi wa Wilaya ya Tarime mkoani Mara, alijaribu kujiua kutoka kwenye daraja hilo lenye urefu wa mita 5.5 na kukimbizwa katika Hospitali ya Rufani Mkoa Sekou-Toure.

"Alijirusha katika kivuko hicho na kuanguka katikati ya barabara Mei 3, 2024 baada ya kumkuta mchumba wake aliyekuwa akimsomesha akiwa na mtoto na mwanamume mwingine na wala hayupo masomoni," amesema kamanda huyo.

Amesema mtuhumiwa huyo alipata majeraha   usoni na mikononi na kupelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu akiwa chini ya ulinzi wa polisi kwa ajili ya mahojiano.

"Vilevile tunaendelea na upelelezi wa tukio hili utakapokamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili," amesema.

Amewataka wazazi na walezi kuacha kuchukua maamuzi kwa mihemuko bali watafute ushauri kutoka kwa viongozi wao wa dini na watu wenye busara badala ya kutoa uhai kwa maamuzi yasiyo sahihi.